Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Mkazi Mhe. Geophrey Pinda ameongoza harambee iliyochangisha Shilingi milioni 132 kwa ajili ya kusaidia Ujenzi wa kituo cha watoto yatima cha "The Joy of God Ophanage Center" kilichopo jijini Arusha.
Hafla ya harambee hiyo imefanyika jana
katika nyumba ya Bushback Safari Kilenge iliyopo mtaa wa Impla jijini Arusha.
Akitoa shukurani kwa wananchi, wadau
pamoja na viongozi wa serikali waliofika katika harambee hiyo Mhe. Pinda
amewasihi Watanzania kujitoa kuwasaidia, kuwalea na kuwajengea makazi watoto
wasio na uwezo wakiwemo yatima.
"Tutakuwa na ushahidi kwamba tuna
kitu tutakifanya, hizi milioni 132 zinakwenda kusaidia watoto hawa wenye
uhitaji maalumu, uhitaji maalum maana yake hawana walezi na sasa tumeamua
kusaidiana na 'Sister' katika kuwalea, kuwanjea makazi na maisha yao kuwa
salama," amesema Mhe.Pinda
Aidha, amezishukuru taasisi zote za
kifedha zilizoshiriki katika harambee hiyo huku akiasa taasisi nyingine kwamba,
bado zina nafasi ya kuchangia ujenzi zaidi wa kituo hicho.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya
Arusha Mhe. Felician Gasper Mtahengerwa amewashukuru wananchi kwa kujitolea kwa
moyo wa dhati katika kuhakikisha wanafanikisha ujenzi wa kituo hicho.
"Niwashukuru sana kwa namna
mlivyoguswa katika utoaji wenu hakika ni jambo la kushukuriwa mno ili kuwalea
vema watoto wetu hawa," amesema Mhe. Mtahengerwa
Naye Mlezi wa kituo hicho Sister
Janeth Ngopa amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt.
Samia Suluhu Hassan kupitia kwa Naibu Waziri wa Ardhi kwa kushiriki na
kuendesha zoezi hilo kikamilifu la uchangiaji ujenzi wa kituo hicho.
"Kwa niaba ya watoto wadhamini na
bodi ya kituo hiki ninamuomba Mungu ampe maisha marefu Mungu, ampe afya njema
na tunamuomba asichoke kutusaidia kwa sababu mara kwa mara tutamsumbua kwa njia
ya simu kutusaidia," amesema Sister Janeth.
0 Maoni