Mikoko kuwanufaisha kimapato wanakijiji Mwaboza

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji ameahidi neema kwa wanakijiji wa Kijiji cha Mwaboza, Kata ya Moa katika Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga, ambao sasa wataanza kupata malipo kwa utunzaji wa miti aina ya mikoko.

Dkt. Kijaji amesema Rais Samia Suluhu Hassan amemtuma kuja Tanga  kuwaeleza wanakijiji wa Mwaboza kuhusu kupatiwa malipo yao ya kutunza mikoko na amewahimiza wasiikate miti hiyo badala yake wapande zaidi mikoko ili wanufaike nayo.

“Hatuhitaji ukate mikoko yako endelea kupanda natunataka uendelee kupokea pesa kwa mikoko yako kwa maisha yako wewe na kizazi chako,” alisema Waziri Dkt. Kijaji na kuongeza, “Hiyo ndio kazi ya Mama (Rais) na ndio maana kanituma nije Tanga niwaambie maneno haya na anawapongeza kwa kutunza mazingira na sasa pesa inakuja.”

Dkt. Kijaji aliyasema hayo wakati akielezea faida ya Utunzaji na Uhifadhi wa Mazingira hasa katika upandaji wa miti aina ya mikoko wakati akiongea na wanakijiji hao jana Oktoba 23, 2024.

FAIDA ZA MIKOKO

-Mikoko inasaidia kupunguza kasi ya mawimbi makubwa ya bahari ambayo yangeweza kufanya uharibifu katika maeneo ya pwani mwa bahari.

-Mikoko pia hutoa mazingira mazuri ya samaki kuzaliana na kukwepa kasi ya mawimbi makali.

-Mikoko inauwezo wa kuhifadhi hewa ya ukaa (carbondioxide) kutoka angani na kuzalisha oksijeni kupitia kitendo cha mmea kiitwacho "photosynthesis".

-Mikoko inachuja maji ya chumvi na kuondoa 90% ya chumvi inayopatikana katika maji ya bahari na kuingia kwenye mizizi yake.

Katika ziara hiyo pamoja na mambo mengine Dkt. Kijaji alikagua, kuzindua na kuweka mawe ya msingi katika miradi ya maendeleo na kufanya mikutano ya kuongea na wananchi mkoani humo. 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji akifafanua jambo mara baada ya kuzindua Shule ya Sekondari Kiomoni iliyopo Kata ya Mzizima, Halmashaurii ya Jiji la Tanga mkoani Tanga.

Chapisha Maoni

0 Maoni