Hakuna mwananchi aliyefukuzwa katika eneo la Loliondo- Serikali

 

Serikali imesema kuwa hakuna mwananchi yeyote anayefukuzwa katika eneo la Loliondo lenye  ukubwa wa kilomita za mraba 2,500 ambalo lilimegwa kutoka pori la akiba Pololeti katika Wilaya ya Ngorongoro ambalo Serikali ililitoa kwa ajili ya shughuli za wananchi.

Akizungumza na waandishi wa Habari jijini Dodoma Msemaji  Mkuu wa serikali na Mkurugenzi wa Idara ya Habari-Maelezo Bw.Mobhare Matinyi  amesema  taarifa hizo hazina ukweli wowote, kwani Serikali ilikabidhi eneo hilo kwa ajili ya matumizi ya Wananchi kufuatia kumegwa kwa lililokuwa  pori tengefu la Loliondo mwaka 2022.

Amebainisha kuwa awali pori hilo lilikuwa na   ukubwa wa kilomita  za mraba 4,000 ambapo baada ya kugawanywa Kilomita za mraba 1,500 ambazo ndio Pori la akiba pololeti  zilibaki kwa ajili ya shughuli za uhifadhi na Kilomita za Mraba 2,500 Serikali ilizitoa kwa ajili ya Wananchi kufanya shughuli zao za maendeleo.

Bw. Matinyi alisisitiza kuwa  serikali itaendelea kusimamia shughuli za uhifadhi katika eneo la Ngorongoro na kuwataka wananchi kupuuza taarifa hizo  kwa kuwa Serikali inatekeleza majukumu yake kwa kuzingatia sheria, kanuni, taratibu na kufuata misingi ya haki za binadamu.

Amewataka wananchi wote wanaoishi katika eneo walilopewa na  Serikali lenye kilomita za mraba 2500 kuendelea na shughuli zao na kupuuza taarifa hizo zenye lengo la kupotosha umma.

Aidha, amesema Serikali itaendelea kuheshimu haki za binadamu katika zoezi la kuhamisha watu wanaojiandikisha kuhama kwa hiyari kutoka eneo la hifadhi ya Ngorongoro kwenda maeneo mengine nchini.

Matinyi amesisitiza msimamo wa Serikali kuwa inawahamisha wananchi wanaojiandikisha wenyewe kuhama katika eneo la hifadhi ya Ngorongoro na kwamba hakuna  ukiukwaji wowote wa haki za binadamu unaofanyika katika utekelezaji wa zoezi hilo.

Ameeleza kuwa serikali ya Tanzania inatekeleza mpango huo ikiamini katika kutimiza malengo ya dunia ya milenia ya kuhakikisha usalama wa watu wake, huduma bora za kijamii ikiwemo elimu, afya na maji huku akisema kwamba serikali itaendelea kuhamasisha wananchi hao kukubali kuhama kwa hiyari.

Bw. Matinyi ameeleza kuwa mtu yoyote au kundi linalotaka kutembelea eneo la hifadhi ya Ngorongoro wanakaribishwa na wanachotakiwa kufanya ni kufuata taratibu ili waweze kuruhusiwa kwa kuwa Serikali haina sababu ya kumzuia mtu yeyote kufika eneo hilo.

Akizungumza hoja ya kuwepo kwa watu asili nchini Tanzania Bw. Matinyi amesema kuwa watanzania wote wanatambulika kwa utaifa wao ambapo kuna zaidi ya makabila 120 na hivyo suala la kuhamisha watu katika hifadhi hiyo lisitazamwae katika kuhamisha kabila fulani bali wananchi wote waliopo huko wanahamisishwa kuhama kadri wanavyojiandikisha.


Chapisha Maoni

0 Maoni