Waziri Mkuu Mhe. Kassim
Majaliwa ameiagiza Wizara wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari,
kufanya uratibu wa madai yote ya vyombo vya habari serikalini ili madeni yao
yaweze kulipwa.
Mhe. Majaliwa ametoa maagizo
hayo jana Mkoani Lindi wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Saba wa Mwaka wa Jukwaa
la Wahariri Tanzania, ambapo amesema madeni hayo yaliletwa ofisi yake na
kuyafanyia uchambuzi.
“Sisi Ofisi ya Waziri Mkuu iliyachambua
madeni yote na wizara zote tuliziandikia barua kali kabisa, na malipo yalianza
kulipwa, lakini zipo wizara sugu ikiwamo hiyo aliyoitaja Mwenyekiti wa Jukwaa
la Wahariri,” alisema Mhe. Kassim Majaliwa.
Kwa hiyo nijukumu lako kuona
tasnia ambayo wewe Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
unailea haipaswi kuendelea kulalamika, alisema Mhe. Majaliwa akionesha kuguswa
na suala hilo.
Mhe. Majaliwa amemtaka Waziri
wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari akutane na mawaziri wenzake,
makatibu wakuu na wakurugenzi wafanye mapitio madai yote kuona yapi yanalipika
ili wanahabari waweze kulipwa madai yao.
“Muweke utaratibu wa kudumu
na ambao ni endelevu ili kutatua changamoto hii, kama mmeweka bajeti kwa ajili
ya vyombo vya habari na ni jambo muhimu wizara haiwezi kukaa kimya lazima
Watanzania wajue, na muache kuwakopa kopo wanahabari,” alisema Mhe. Majaliwa.
Pia, ameiagiza Wizara wa
Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kukamilisha mchakato wa kuandaa
kanuni za Sheria ya Huduma za Habari, na maeneo yote yanayohusiana na sheria
hiyo hiyo ili ianze kufanyakazi.
Awali, Mwenyekiti wa Jukwaa
la Wahariri Tanzania (TEF) Deodatus Balile alimshukuru Waziri Mkuu wa kuagiza
kulipwa madai ya vyombo vya habari, ambapo baadhi yamesha lipwa ila ya Wizara
ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) bado hayajalipwa.
0 Maoni