Kampuni binafsi za ulinzi zisizonasifa zapigwa marufuku

 

Jeshi la Polisi nchini limezitaka kampuni binafsi za ulinzi zisizo na sifa ya kutoa huduma ya ulinzi kusitisha mara moja hadi zitakapokidhi vigezo.

Marufuku hiyo imetolewa na Mkuu wa usimamizi wa kampuni binafsi za ulinzi kutoka makao makuu ya jeshi la polisi Kamishna msaidizi mwandamizi wa polisi (SACP) Urich Matei akiwa jijini Mwanza kwenye kikao kazi kilicholikutanisha jeshi hilo na wamiliki na wasimamizi wa kampuni binafsi za ulinzi.

SACP Matei amempongeza Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza Wilbroad Mutafungwa kwa hatua ya kufanya vikao vya mara kwa mara na wamiliki wa makampuni hayo na kuweka mikakati ya kuhakikisha wanafanya shughuli zao kwa ufanisi.

"Natoa pongezi za dhati kwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Wilbrod Mutafungwa kwa kikao alichokifanya wiki mbili zilizopita nilikiona kupitia vyombo vya habari kati ya Jeshi la Polisi na kampuni binafsi za ulinzi kilikuwa kizuri sana," amesema SACP Matei.

Ameongeza "Aliweka mikakati ambayo wote tumezingatia ili kukabili changamoto zinazotukuta, hongereni sana.”

Katika hatua nyingine SACP Matei ametoa rai kwa Makamanda wa Polisi nchini kuiga mfano wa Kamanda Mutafungwa na timu yake kwa kufanya vikao na kampuni binafsi za ulinzi.

"Nitoe rai kwa makamanda wote wa Jeshi la Polisi nchini, kupitia kitengo cha Polisi Jamii watoke ofisini na wasaidizi wao kwenda kwenye maeneo yao ili kupata takwimu sahihi ya kampuni zinazofanya kazi kwenye maeneo yetu na askari wanaolinda pamoja na kumbukumbu zao" amesema Matei.

Kwa upande wake, Afisa Polisi Jamii Mkoa wa Mwanza, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Ramadhani Sarige ameahidi kuendeleza usimamizi thabiti kwa kampuni hizo ikiwa ni pamoja na kuchukua hatua za kisheria kwa kampuni zitakazo shindwa kufuata sheria

Amani Nasoro ni Mkurugenzi wa Kampuni binafsi ya ulinzi ya Amaka ameliomba Jeshi la Polisi nchini kuanzisha kitengo cha kutoa elimu kwa walinzi wa kampuni binafsi za ulinzi ili kuwa na watendaji wanaofanana kama askari Polisi walivyo Mikoa yote.

 "Askari wa Mkoa wa Katavi na wa Mwanza wako sawa kiutendaji lakini askari wa kampuni binafsi za ulinzi hawafanani kiutendaji kutokana na tofauti  ya mafunzo wanayoyapata sehemu tofauti," amesema Amani.



Chapisha Maoni

0 Maoni