Naibu Waziri Mkuu na Waziri
wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko leo amezindua kituo cha kwanza cha kisasa cha
kujazia gesi asilia kwenye magari na karakana ya kuweka mfumo wa gesi asilia
ikiwa ni muendelezo wa utekelezaji wa mipango ya Serikali kuchochea matumizi ya
gesi asilia kama nishati safi na salama kwa mazingira.
Uzinduzi huo umefanyika
jijini Dar es Salaam jana na kuhudhuriwa na Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward
Mpogolo, Balozi Sherif Ismail wa Jamhuri ya Kiarabu ya Misri, Balozi Isaac
Njenga wa Jamhuri ya Kenya, Balozi Fred Mwesigye wa Jamhuri ya Uganda, Mha.
Felchesmi Mramba, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Mtendaji Mkuu wa kampuni
ya TAQA, Pakin Kafafy.
Dkt. Biteko amesema kuwa,
kujengwa kwa kituo hicho na TAQA Arabia na washirika wao JCG Oil & Gas
niutekelezaji wa maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.
Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa na maono ya kuleta wawekezaji nchini
wakiwemo wanaowekeza kwenye Sekta ya Nishati, hivyo ameahidi kuwa Wizara itafanyia
maelekezo yake ili kutekeleza maono yake.
Dkt. Biteko amesema kuwa,
Serikali inaweka msukumo mkubwa kwenye matumizi ya gesi ya asilia yakiwemo
magari, mitambo ya viwandani, hivyo kuzinduliwa kwa kituo hicho ni kuonesha
azma ya Serikali ya kuhakikisha kuwa Gesi inayopatikana Tanzania inatumika
ndani ya nchi kwanza.
Amesema kituo hicho kitajaza
gesi kwenye magari 800 kwa siku na kina pampu sita zitakazojaza gesi kwenye
magari sita kwa maramoja ambapo ujazaji wa gari moja utakuwa ni wa dakika tatu
hivyo hicho ni kituo kikubwa kitakachosaidia kubadilisha magari na kufanya
yatumie gesi badala ya mafuta pekee.
Amesema Kampuni hiyo
inatarajia kujenga vituo 12 vya CNG jijini Dar es Salaam ili kuwa na vituo
vingi zaidi vya kujazia gesi kwenye magari.
Ameongeza kuwa, kampuni hiyo
kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) wapo kwenye
majadiliano ili kujenga vituo vidogo vya Gesi ya Kusindika (LNG) ili kuweza
kutoa Gesi jijini Dar es Salaam na kupeleka kwenye mikoa mbalimbali ili nayo
iweze kujaza gesi hiyo kwenye magari.
Amesema kuwa Serikali
itaendelea kuwaunga mkono katika uwekezaji wao ili kuchochea ukuaji wa nishati
nchini.
Kwa upande wake, Mkuu wa
Wilaya ya Ilala, Mhe. Edward Mpogolo ameishukuru Wizara ya Nishati kwa
kutekeleza maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu
Hassan ya usambazaji nishati katika maeneo yote ikiwemo gesi asilia.
Amesema kuwa Wilaya ya
Ilala, inaona faraja kufunguliwa kwa kituo wilayani humo kutokana na kuwa
kitovu cha Mkoa wa Dar es Salaam kwani Wilaya hiyo ina wananchi wasiopungua
milioni 1.6 ukilinganisha na idadi yote ya wakazi wa Mkoa wa Dar es Salaam
ambao jumla yao ni milioni 5.3.
0 Maoni