Mkazi wa Nyasaka wilayani
Ilemela mkoani Mwanza, Philipo Mhina (52), amefikishwa katika Mahakama ya
Hakimu Mkazi Wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza na kusomewa shtaka la kuendesha
gari kwa uzembe katika barabara ya Umma na kusababisha kifo cha askari wa
Usalama Barabarani, WP 3984. Sajenti, Stella Alfonce.
Philipo amesomewa shtaka
hilo leo Novemba 10, 2023 katika kesi ya jinai namba 36752/2023 ambapo anadaiwa
kutenda kosa hilo kinyume na kifungu namba 41, 63 (2) (b) na 27 (1) (a) cha
Sheria ya Usalama Barabarani sura 168 marejeo ya mwaka 2002.
Mbele ya Hakimu Mkazi
Mwandamizi Amani Sumari, Mwendesha Mashtaka wa Serikali Monica Mweli amesema
mshtakiwa alitenda kosa hilo Novemba Mosi, 2023 eneo la Nyamhongoro wilaya ya
Ilemela.
Mhina ambaye ni dereva wa
gari ya Shule ya Msingi Nyamuge ya jijini Mwanza akiwa anarudisha nyuma gari
hiyo yenye namba za usajili T.964 BRJ aina ya Mitsubishi Rosa baada ya
kukamatwa na kosa la usalama barabarani alimgonga Sajenti Stella na kusababisha
kifo chake.
Baada ya kusomewa shtaka
hilo, mshtakiwa amekana na kurejeshewa rumande kutokana na kutokidhi vigezo vya
dhamana ambapo alitakiwa kuwa na wadhamini wawili na barua ya Mwenyekiti wa Serikali
ya Mtaa kila mmoja.
Hakimu Sumari, ameahirisha
shauri hilo hadi Novemba 23 litakapokuja kwa ajili ya kusomewa maelezo ya awali.
0 Maoni