Mikataba Mitatu ya Uwekezaji Bandari ya Dar yasainiwa

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh. Samia Suluhu Hassan, ameshuhudia utiaji saini wa mikataba mahususi mitatu ya uwekezaji na uendelezaji wa Bandari ya Dar es Salaam katika hafla iliyofanyika katika Ikulu ya Chamwino Jijini Dodoma.

Mikataba hiyo ya uwekezaji baina ya Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) na Kampuni ya DP World ya Dubai ni pamoja na Mkataba baina ya Serikali, Mkataba Uendeshaji Gati namba 4 hadi namba 7 pamoja na Mkataba wa Upangishaji Gati namba 4 hadi namba 7.

Akiongea katika hafla hiyo iliyohudhuriwa pia na Rais wa Zanzibar Dk. Hussein Mwinyi, Rais Samia amesema katika makubaliano hayo maslahi mapana ya nchi yamezingatiwa na kuwahakikishia Watanzania kwamba maoni yao yote mazuri waliyoyatoa yamezingatiwa kwenye mikataba hiyo.

“Serikali ilisikiliza michango na maoni mbalimbali iliyotolewa na Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Vyama vya Siasa, Asasi za Kiraia, Wanaharakati Huru, Vyombo vya Habari na pia tumeangalia pia maoni yaliyotolewa kwenye mitandao ya jamii,” amesema Rais Samia na kuongeza “Tumewasikiliza pia Viongozi wetu wa dini  na baadhi ya Viongozi wetu wastaafu, tumefuatilia kwa karibu sana hoja za Waheshimiwa wabunge wakati wa kujadili na kupitisha azimio la bunge na tulipokea pia ushauri wa Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya CCM.”

Amesema Bandari ya Dar es Salaam ni moja ya kiunganishi muhimu cha kibiashara kati ya Tanzania na mataifa mengine, kwa kuwa inahudumia shehena kubwa ya mizigo ya nchi jirani na hata mataifa ya mbali, hivyo maboresho yakiutendaji yatayofanywa kwa uwekezaji huu yatakuza biashara za ndani na nje na kuchangia katika uchumi wa taifa.

Awali wakati akimkaribisha Rais Samia, Makamu wa Rais Dkt. Philip Mpango alisema kuwa uwekezaji huo ni muhimu kutokana na ukweli kwamba Bandari ya Dar es Salaam inakabiliwa na ushindani wa bandari ya Mombasa Kenya, Msumbiji, Afrika Kusini pamoja na nyingine Afrika ya Magharibi.

“Bandari yetu ispokuwa na tija biashara inakwenda huko kwingine, kwa hiyo ni lazima tujidhatiti tupambane kiushindani, na tukio hili la leo Mheshimiwa Rais wewe ni jasiri kweli kweli, tukio la leo ni kuipeleka nchi yetu ili tukashindane kibiashara kwenye bandari.” alisema Dk. Mpango.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) Plasduce Mbossa alisema kuwa mkataba wa DP World wa uendelezaji na uendeshaji wa Bandari ya Dar es Salaam ni wa miaka 30 na utendaji kazi wa DP World utakuwa ukipimwa kila baada ya miaka mitano.

Chapisha Maoni

0 Maoni