Makonda awatumia salamu Mawaziri na Wakuu wa Mikoa

 

Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC), Itikadi na Ueneza Bw. Paul Makonda, amewatumia salamu Mawaziri, Wakuu wa Mikoa pamoja na Watendaji wote wa Serikali kuwa chama hakitosita kuwachukulia hatua iwapo watabainika hawajafanya kazi yao kikamilifu.

Bw. Makonda ametoa kauli hiyo leo Jijini Dar es Salaam, wakati walipopokelewa katika Ofisi za Ndogo za CCM Lumumba, baada ya kuteuliwa katika nafasi hiyo tarehe 22/11/2023 pamoja Rabia Abdallah Hamid Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Siasa na Mahusiano ya Kimataifa.

“Ninatuma salamu kwa Mawaziri na Wakuu wa Mikoa wote, kuwa kila mtu ataubeba msalaba wake na kwa bahati nzuri tunajuana,” alisema Makonda na kuongeza “Sitakuwa msemaji wa chama muongo, sijafunzwa kwa miaka mitatu na miezi mitatu ili nije kusema uongo.”

Akizungumza kwa mara ya kwanza baada ya kupotea kwenye medani za kisiasa kwa muda wa miaka mitatu na miezi mitatu, Bw. Makonda amesema kiongozi yeyote atakayebainika kuzembea katika kutekeleza majukumu yake CCM itamchukulia hatua.

Kuhusu suala la baadhi ya watu kudhani kuwa baada ya kuteuliwa kwenye nafasi hiyo kuwa atalipa kisasi, Makonda amewatoa hofu kwa kusema “Mimi sina kisasi na mtu yeyote na asiwepo mtu akafikiri lengo langu litakuwa ni kumkandamiza.”

Akiongelea kuhusu watu waliokuwa wanawaza kuwa Makonda atakuja na mambo gani, amesema kwamba yeye hana ya kwake, anayo ya CCM ambayo yanaongozwa na Mwenyekiti wa CCM Taifa Rais Samia Suluhu Hassan.

“Ninajua kuwa Watanzania wanatufuatilia katika vyombo vya habari, na wengi wanataka kujua leo Makonda atasema nini na wengine wameenda mbali zaidi na kusema tuone dira, maono na shabaha yake,” alisema Makonda na kuongeza, “Nataka niwaeleze kuwa hakuna maono ya Makonda, kuna maono na malengo ya CCM, tuna Ilani yenye zaidi ya kurasa 300 jukumu letu ni kuitekeleza na kuielezea.”

Kuhusu upinzani Bw. Makonda amedai kuwa Tanzania haina chama cha upinzani ila inawatoa taarifa waliojikusanya katika vyama vya watoa taarifa, “Tanzania haina chama cha upinzani, Tanzania inawatoa taarifa. Ukimuona Tundu Lissu anaongea sio chama ni mtu tu anatoa taarifa”.

Kuhusu mikutano ya hadhara, Makonda amesema amemuona Mwenyekiti wa Chadema Taifa Freema Mbowe akihutubia mikutano kwa kutumia Helkopta, hii inatokana na dhamira ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kukuza Demokrasia na Uhuru wa watu kujieleza.

Aidha, Bw. Makonda amesema kwa utumia mamlaka aliyonayo anawaagiza wanaohusika na mamlaka ya vibali wampee Mbowe kibali cha kuruka na helkopta na kama ameishiwa na mafuta aseme tu kwa kuwa tayari ameshamuombea kwa Mhe. Rais Samia na amekubali kumchangia mafuta.

Chapisha Maoni

0 Maoni