Hifadhi ya Taifa Tarangire yakabidhiwa vifaa kuimarisha shughuli za Uhifadhi

 

Taasisi ya Marafiki wa Serengeti (Friends of Serengeti Switzerland) wamekabidhi vifaa mbalimbali kwa Hifadhi ya Taifa Tarangire vyenye thamani ya TZS Milioni sabini na tano (75,000,000/-) yakiwemo Mahema, miwani ya usiku (Night Vision Goggles), kiona mbali (Binoculars), "GPS", mafuta (Diesel) pamoja na vifaa vya kuwekea taka ngumu kwa ajili ya kufanikisha na kuimarisha shughuli za Uhifadhi.

Makabidhiano hayo yamefanyika tarehe 24.10.2023 Makao Makuu ya Hifadhi ya Taifa Tarangire, mkoani Manyara.

Akizungumza katika makabidhiano hayo Mwakilishi wa Taasisi ya Marafiki wa Serengeti Switzerland, Suzan Peter Shio alisema kama taasisi wamekuwa na mwendelezo wa kutoa vifaa mbalimbali kwa ajili ya Uhifadhi kwenye hifadhi tofauti tofauti na leo ni Hifadhi ya Taifa Tarangire.

"Pasipo Uhifadhi hamna Utalii, nina imani vifaa hivi vitawasaidia na kuwaongezea ari askari pale wanapokuwa katika shughuli zao za kila siku," alisema Shio.

Akifafanua zaidi, miwani hizi za usiku (night vision goggles) ni za kisasa, mkiwa doria usiku zitawasaidia sana kuwatambua majangili kwa karibu na kwa urahisi, pili mafuta yatawasaidia katika doria zenu za kila siku na shughuli za mipaka. Vifaa hivi vya kuwekea taka ngumu ni vya vituo vyote saba ili kutunza Mazingira ya Hifadhi.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi, Betrice M. Kessy Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Tarangire amewashukuru Marafiki wa Serengeti kwa vifaa vyote walivyotoa vitasaidia kuimarisha shughuli za doria na Uhifadhi.

"Nina furaha kupokea vitendea kazi hivi, kikubwa kabisa ni miwani za kisasa za usiku (night vision goggles) kwa kuwa majangili wengi huingia hifadhini wakati wa usiku, hii itatusaidia kuwaona na kuwakamata kiurahisi, " alisema Kessy.

Aliongeza kuwa mafuta nayo yatasaidia sana kwenye shughuli za doria za mchana na usiku pamoja na matengenezo ya barabara za mipakani, kuzunguka hifadhi ili mipaka yote ionekane vizuri.

"Mipaka itaonekana bayana hivyo wananchi waheshimu mipaka na waache vitendo vya ujangili," alisema Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi Kessy.

Kamishna Kessy alisema Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) linashukuru na linatambua mchango mkubwa unaotolewa na Taasisi ya Marafiki wa Serengeti ambao tangu mwaka 1984 wamekuwa wakitekeleza miradi mingi katika Hifadhi za Taifa Tanzania.

Na. Brigitha Kimario -Tarangire

Chapisha Maoni

0 Maoni