Wakatazwa kutumia gari la wagonjwa kwa matumizi mengine

 

Waziri wa Nchi, Ofisi Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Kibakwe, Mhe.George Simbachawene ameutaka Uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa kuacha kulitumia gari la kubebea wagonjwa (Ambulance) la Kituo cha Afya cha Rudi kwa matumizi mengine badala yake gari hilo litumike kwa lengo lililokusudiwa ili kusaidia kupunguza vifo vya akina mama wajawazito na wagonjwa wengine pindi linapohitajika.

Amesema ni aibu kuona gari ya kubebea wagonjwa likitumika kwa ajili ya kufanyia mambo mengine huku kusudio la msingi wa gari hilo llikiwa limeachwa huku akina mama wajawazito na wagonjwa wengine mahututi wakihatarisha maisha yao.

Mhe. Simbachawene ameyasema hayo wakati akizungumza na wananchi wa Kata ya Rudi katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Shule ya Msingi ya Chilendu, Jimbo la Kibakwe katika Wilaya ya Mpwapwa mkoani Dodoma, ikiwa ni ziara yake ya kimkakati ya kukagua utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi

Amesema malalamiko ya wananchi walio katika hali duni ni mengi kuhusu matumizi ya gari hilo, kusudio la gari hili ilikuwa ni kuwasaidia wagonjwa walioshindwa kutibiwa katika Kituo hicho cha afya waweze kukimbizwa katika Hospitali ya juu zaidi ili kuokoa maisha yao lakini muda mwingi gari hilo limekuwa likitumika kwa shughuli zingine katika Halmashauri ya Mpwapwa ambako ni mbali na kituo kilipo.

"Unakutana na gari la kubebea Wagonjwa limebeba maofisa wa Halmashauri ilhali huku wagonjwa wanaohitaji kusafirishwa kwa matibabu zaidi wakilazimika kukodi gari kutoka kwa watu binafsi, jambo hili halikubaliki," amesema Mhe.Simbachawene.

Aidha, Mhe.Simbachawene ametaka gari hilo liwepo saa 24 katika Kituo hicho cha Afya badala ya kuliweka katika ofisi za Halmashauri ya Wilaya Mpwapwa kwa madai kuwa hakuna wagonjwa wanaolihitaji.

Ameutaka Uongozi huo wa Halmashauri kujitathmini kama wapo pale kwa ajili ya kuwahudumia wananchi kwani haiwezekani wananchi wakiachwa wanataabika na muda mwingine hupoteza maisha ilhali gari lipo ila linatumika kwa matumizi yasiyo yake.

Kwa mujibu wa wananchi, licha ya kujitahidi kutumia nguvu zao kujenga sehemu maalum ya kuhifadhia gari hilo la wagonjwa katika kituo hicho cha afya lakini gari hilo muda mwingi limekuwa halikai hapo.

Katika hatua nyingine, Mhe.Simbachawene ametoa wito kwa akina mama wajawazito kuwahi katika vituo vya afya mara waonapo dalili za kuanza kwa uchungu ili kuepuka vifo visivyo vya lazima huku akiwasihi manesi kuwahudumia wagonjwa kwa upendo kama viapo vyao vinavyowataka

Chapisha Maoni

0 Maoni