Serikali kupitia Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia,
Wanawake na Makundi Maalum imeihimiza jamii kote nchini kukumbuka ujenzi wa
makazi ya wazee wasiojiweza wakati huu wa mabadiliko ya sayansi na teknolojia.
Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii,
Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Mwanaidi Ali Khamis wakati akishiriki
katika shughuli za maendeleo Wilayani Tarime mkoani Mara.
Akiwa kwenye ujenzi wa nyumba ya daktari wa zahanati ya Kijiji
cha Soroneta amesema Jamii inatakiwa kushiriki katika shughuli za maendeleo ili
wawe na umiliki wa miradi hiyo hususan suala la utunzaji ili idumu.
Mwanaidi amesema, Kampeni ya Amsha Ari ni moja ya juhudi za
Serikali kupitia Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi
Maalum juu ya utekelezaji wa Sera ya Maendeleo ya Jamii ya Mwaka 1996
inayohimiza Wananchi kujitolea wakati wa shughuli za maendeleo kwenye maeneo
yao.
"Mimi nimekuja hapa kuamsha ari ya wananchi kuweza
kujenga makazi bora na pia kusaidia watu wengi kuwa na makazi bora hasa wazee
wasio na uwezo" amesisitiza Naibu Waziri Mwanaidi.
Naye Diwani wa Kata ya Nyarelo Japheth Marwa, amesema wananchi wa kata hiyo
wamekuwa na moyo na ari ya kujitolea katika shughuli za maendeleo na
wataendelea kujitoa ili kufanikisha miradi mbalimbali ya huduma za jamii iweze
kuwasaidia kuondokana na changamoto zinazowakabili
Kwa upande wake, Mganga Mfawidhi wa Zahanati ya Kijiji cha Soroneta
Kata ya Nyarelo Dkt. Richard Kitende ameishukuru Serikali kwa kuunga mkono
juhudi za wananchi kutekeleza miradi ya Maendeleo kwani inasaidia kuwapa moyo
wa kujitoa na kusaidia upatikanaji wa huduma muhimu karibu na maeneo yao.
Akizungumzia hatua hiyo, Mbunge wa Tarime Vijijini Mwita
Waitara amesema ni jambo jema viongozi kuonesha mfano kwenye masuala ya
maendeleo na jamii kwani itasaidia kuwa na moyo na mwamko kwa wananchi
kuchangua katika shughuli za maendeleo.
Awali, Afisa Maendeleo ya Jamii Janeth Michael alisema mradi
huo umeshirikisha wananchi kwa shughuli za kuchimba msingi, kusomba mawe na
kujenga boma ambapo gharama zote za nguvu ya wananchi ni shillingi Millioni 8.1
huku wakiungwa mkono na Halmashauri ya Wilaya ya Tarime iliyotoa shillingi
Millioni 20 kuunga mkono juhudi za Wananchi.
Na. WMJJWM- Tarime, Mara
0 Maoni