Madaktari na Walimu wasisimamie miradi ya ujenzi

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.George Simbachawene (Mb) ametaka   Madaktari na Walimu wasiwe wasimamizi wa miradi ya ujenzi inayotekelezwa katika maeneo yao ya kazi huku akisisitiza kuwa sio taaluma yao na ni matumizi mabaya ya rasilimaliwatu.

Badala yake, ameutaka Uongozi wa Halmashauri zote nchini hususan Halmashauri ya Mpwapwa kuhakikisha inaachana utaratibu huo, iajiri Wataalam wa fani ya ujenzi kwa ajili ya kusimamia miradi yote itakayokuwa ikitekelezwa katika Halmashauri hiyo ili iwe ya viwango vya ubora kama ambavyo baadhi ya Halmashauri zingine zinafanya.

Ameyasema hayo mwishoni mwa wiki wakati akikagua ujenzi wa mradi wa vyumba viwili vya maabara wenye thamani ya Shilingi milioni 60 unaoendelea katika Shule ya Sekondari Rudi iliyopo katika Jimbo la Kibakwe, Halmashauri ya wilaya ya Mpwapwa, Mkoani Dodoma, ikiwa ni ziara ya kukagua utekelezaji wa miradi ya ujenzi katika Jimbo hilo.

" Kwa sasa majengo yetu yanajengwa na Walimu na Madaktari na badala ya kujengwa na Wahandisi wa ujenzi, hili halikubariki hata kidogo, amesititiza Mhe.Simbachawene.

Ameweka angalizo kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa imekuwa haifanyi vizuri katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya ujenzi kutokana na usimamizi hafifu kwa sababu Wasimamizi wanaopewa jukumu hilo sio taaluma yao.

Amefafanua kuwa Walimu au Madaktari wanaosimamia miradi hiyo ujenzi sio kwamba ni wabadhirifu lakini kwa kuwa sio taaluma yao hivyo ni vigumu kuona na hata kushauri pale ujenzi unavyojengwa chini ya kiwango.

Amesema limekuwa ni jambo la kawaida kama mradi afya unatekelezwa basi msimamizi wa ujenzi atakuwa Daktari, vivyo hivyo kama ujenzi wa madarasa basi msimamizi atakuwa Mwalimu.

" Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ajirini wataalamu wa ujenzi hata kwa ajira ya mkataba ili waweze kusimamia ujenzi haiwezekani Miradi yetu isimamiwe na Walimu na Madaktari kwani wao sio Wahandisi wa majengo,” alisema Mhe. Simbachawene.

Ameongeza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan moja ya msisitizo wake katika itekelezaji wa miradi ni lazima iendane na thamani ya fedha.

Katika hatua nyingine, Mhe.Simbachawene amewasihi madiwani ya Halmashauri ya Mpwapwa kujiepusha na tabia ya kuchukua tenda ya miradi ya ujenzi inayotekelezwa ndani ya Halmashauri hiyo ili kuepusha mgongano wa maslahi baina yao.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Mhe.Richard Maponda amesema atahakikisha wanasimamia maelekezo hayo ili kodi za watanzania zinazotumika katika kutekeleza miradi hiyo iendane na thamani halisi ya fedha.

Chapisha Maoni

0 Maoni