Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), limeonya
tabia iliyoanza kuibuka kwa siku za hivi karibu ya wimbi kubwa la wananchi
wanaovaa sare zinazofanana na za JWTZ ama mavazi yanayofanana na sare za
kijeshi.
Kaimu Mkurugenzi wa Habari na Uhusiano Makao Makuu ya JWTZ, Luteni
Kanali Gaudentius Gervas Ilonda, amesema kumekuwa na wimbi kubwa la baadhi ya
wananchi wanaokamatwa au konekana wakiwa wamevaa sare za JWTZ ama mavazi
yanayofanana na sare za kijeshi.
"Nimewaita waandishi wa habari leo ili kupitia kwenu
JWTZ liweze kutoa taarifa kuhusiana na kadhia hiyo inayokizana na katazo la
kisheria la raia kuvaa, kumiliki au kuuza mavazi ya kijeshi au yanayoelekea
kufanana na sare za jeshi," alisema Luteni Kanali Ilonda.
Amesema kwamba sheria inakataza mavazi hayo ambayo ni pamoja
na kombati (vazi la mabaka mabaka), makoti, t-sheti, suruali, magauni, kofia,
viatu, mabegi na kaptura zenye rangi zinazofanana ua kushonwa katika mitindo ya
kijeshi.
Luteni Kanali Gaudentius Gervas Ilonda, amesema kwamba
katazo hilo ni kwa mujibu wa kifungu cha 99 cha Sheria ya Ulinzi wa Taifa (NDA)
sura ya 192 Sheria namba 24 ya mwaka 1966 iliyofanyiwa marejeo mwaka 2002.
Ameongeza kwamba, kifungu cha 178 cha Sheria ya Kanuni ya
Adhabu Sura ya 16 (Penal Code) na kifungu cha 6 cha Sheria ya Usalama wa Taifa,
vinakataza raia kuvaa sare na mavazi ya majeshi ya ulinzi au yanayofafana nayo.
Amesema kwamba zipo baadhi ya taasisi zinazowashonea
watumishi wake sare za aina hiyo na wapo pia baadhi ya wafanyabiashara
wanaoingiza nchini mavazi ya aina hiyo na kuyauza kwa raia kupitia maduka yao
ama maeneo yao ya biashara.
Ameeleza kuwa wapo pia baadhi ya wasanii wanaovaa mavazi
hayo na kuyatumia wawapo kwenye majukwaa ya kazi zao bila kufuata utaratibu.
Pia, amesema wapo baadhi ya wananchi wamekuwa wakiyatumia kufanya vitendo vya
uvunjifu wa sheria na kudhaniwa kuwa ni wanajeshi.
0 Maoni