DC Ulanga awataka vijana kulinda amani kwa maendeleo ya taifa

 

Mkuu wa Wilaya ya Ulanga, Khamana Juma Simba, amewahimiza vijana wa wilaya hiyo kulinda amani ya taifa ili kila mwananchi awe huru kufanya shughuli zake za maendeleo, akisisitiza kuwa maendeleo hayawezi kupatikana bila kuwepo kwa amani.

Simba alitoa kauli hiyo wakati wa uzinduzi wa Jukwaa la Vijana (Youth Platform), linalolenga kuwakutanisha vijana kutoka makundi mbalimbali kwa ajili ya kujadili masuala ya maendeleo na fursa zinazowahusu.

“Mimi niwaombe vijana wa Wilaya ya Ulanga kutoka maeneo yote twende tukawa walinzi wa wilaya yetu, nendeni mkawa walinzi wa nchi yetu na walinzi wa sisi wenyewe, tutapunguza mambo yote mabaya,” alisema Simba.

Aidha, aliwataka vijana kutumia fursa za mikopo zinazotolewa na Halmashauri kwa ajili ya kujiendeleza kiuchumi na kujenga maisha bora, huku akiwahimiza kuwa mabalozi wazuri kwa wenzao katika jamii.

Pia, aliwaasa vijana kutotumia vibaya mitandao ya kijamii, badala yake waitumie kama chombo cha kujifunza, kufanya biashara na kujiongezea kipato.

“Mitandao ya kijamii inaweza kuwa nyenzo muhimu ya maendeleo ikiwa itatumika kwa malengo chanya. Wapo watu wanaofanya biashara kupitia mitandao hiyo na kupata riziki zao,” alisema.

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Ulanga, Salim Hashim, aliwataka vijana kuchangamkia fursa mbalimbali zinazopatikana kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Ulanga ili kujikwamua kiuchumi.

Hashim alisema ofisi yake imeandaa mpango maalumu wa kuwawezesha vijana kupitia mikopo isiyo na riba, hatua inayolenga kuwasaidia kukuza na kuendeleza biashara zao pamoja na shughuli nyingine za uzalishaji mali.

Alisisitiza kuwa uwezeshaji wa vijana kiuchumi ni moja ya njia muhimu za kupunguza changamoto za ajira na kuongeza ushiriki wao katika maendeleo ya wilaya na taifa kwa ujumla.

Chapisha Maoni

0 Maoni