Kihongosi: Wanaochochea machafuko Afrika hutumiwa kwa maslahi binafsi

 

Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM anayeshughulikia Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Kenani Kihongosi, amesema sehemu kubwa ya machafuko na migogoro inayoshuhudiwa katika baadhi ya nchi za Afrika huchochewa na watu wachache wanaotumiwa kwa maslahi binafsi ili kuvuruga amani na utulivu wa mataifa yao.

Kihongosi alitoa kauli hiyo wakati akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika eneo la Kilombero, jijini Arusha, Mei 7, alipokuwa akihitimisha ziara yake mkoani humo.

Alisema historia inaonyesha kuwa hata wakati wa ukoloni kulikuwepo watu waliotanguliza maslahi yao binafsi na kushiriki katika vitendo vilivyowadhuru Waafrika wenzao kwa manufaa ya fedha na madaraka.

“Kuna watu wanalipwa fedha nyingi kwa ajili ya kuchochea migogoro ndani ya bara la Afrika. Ndiyo maana hata wakati wa ukoloni walikuwapo wasaliti waliowauza Waafrika wenzao kwa kupewa vipande vya fedha na madaraka,” alisema Kihongosi.

Aliwataka wananchi kuwa makini na watu wanaotumia mbinu mbalimbali kupotosha ukweli na kueneza chuki katika jamii kwa malengo ya kuvuruga mshikamano wa kitaifa.

Kihongosi alisema ni muhimu kwa wananchi kuendelea kudumisha umoja, upendo na mshikamano ili kulinda amani ambayo ni msingi wa maendeleo ya nchi.

Aidha, alionya dhidi ya matumizi mabaya ya majukwaa ya kisiasa, akisema baadhi ya wanasiasa wamekuwa wakiyatumia kueneza chuki na kuhamasisha machafuko, jambo ambalo linaweza kuhatarisha maendeleo na ustawi wa jamii.

Alisisitiza kuwa siasa zinapaswa kutumika kama chombo cha kujenga maridhiano, kuhimiza maendeleo na kuimarisha mshikamano wa wananchi badala ya kuzalisha migawanyiko ndani ya jamii.

Chapisha Maoni

0 Maoni