Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametoa wito kwa jamii kuwa walinzi wa watoto na kujijengea utamaduni wa kutoa taarifa vinapotokea vitendo vya ukiukwaji wa maadili.
Waziri Mkuu Majaliwa ameyasema hayo leo jijini Dar es Salaam katika hafla ya mtoko na mama ambapo amesisitiza maadili ndio utambulisho wa kila mmoja katika jamii.
“Watanzania wote tushirikiane kukemea vikali vitendo vyote vya mmomonyoko wa maadili kwa kisingizio chochote,Mkataa kwao ni Mtumwa, sisi ni watu huru” amesema Waziri Mkuu Majaliwa
Aidha amewasihi Viongozi wa madhehebu ya dini kuendelea kuwalea watoto kiroho na kuwahimiza kuacha vitendo visivyofaa kwa kuwa havimpendezi Mwenyezi Mungu.
“Suala la malezi bora yanayofuata Maadili, Mila na Desturi tulizozirithi kutoka kwa wazee wetu ni jambo muhimu na linapaswa kuendelezwa na kulindwa na kila mmoja ili kujenga Taifa bora”
Ameitaka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum kufanya uhamasishaji kwa jamii, ili miongozo yote iliyoandaliwa ilete tija iliyokusudiwa kwa jamii.
“Ninatambua kuwa mama zetu katika karne hii mnafanya shughuli nyingi za kiuchumi kwa ajili ya ustawi wa familia na Taifa kwa ujumla. Niwasihi sana muendelee kuwa vinara katika suala la malezi ya watoto”
Amesema Serikali imeendelea kujenga mazingira bora ili kuleta usawa katika upatikanaji wa elimu. Suala la elimu ya mtoto wa kike ili kuwa na mama bora limepewa kipaumbele kikubwa na Serikali ya Awamu ya sita kupitia utekelezaji wa afua mbalimbali
Wazazi wote wawili ndio msingi wa malezi bora kwa watoto wetu na wanao wajibu wa kuhudumia familia kulingana na mgawanyo wa majukumu waliyonayo
0 Maoni