Mgomo wa wafanyabiashara Kariakoo ngoma ngumu

 


Mgomo wa wafanyabiashara wa Kariakoo huenda ukaendelea kwa siku kadhaa licha ya jitihada za Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Amos Makalla kuingilia kati hii leo kujaribu kuutuliza, lakini inaonekana jitihada hizo zimegonga mwamba.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Makalla amekutana na wafanyabiashara hao na kuwataka kusitisha mgomo huo, lakini wafanyabiashara huenda wakaendelea na mgomo huo hadi Ijumaa, sasa wakitaka kukutana na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan.

Mgomo huo wa wafanyabiashara wa Kariakaoo umenza leo jumatatu, ambapo wamefunga maduka yao kwa ajili ya kushinikiza serikali kuingilia kati utitiri wa kodi wanaotozwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Msimamo wa kuendelea na mgomo huo, umeonekana kwenye kikao na Mkuu wa Mkoa Makalla ambapo walionekana kutoridhika na maelezo yake, na hata aliposema Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa atafanya kikao na kamati ya wafanyabiashara wa soko hilo siku ya Alhamisi Dodoma.

Baadhi ya wafanyabiashara wamesema iwapo wanataka wafungue maduka na kufanya biashara ni vyema watimize lengo lao la kukutana na Rais Samia Suluhu Hassan ili wamueleze madhili wanayopitika wafanyabiashara na si mkuu wa mkoa.

Iwapo msimamo huo wa mgomo utaendelea hadi Ijumaa utasababisha athari za kiuchumi, kutokana na eneo hilo la Kariakoo, kuwa ni kitovu cha biashara nchini, likitegemewa zaidi na mikoa mingine na hata wafanyabiashara kutoka nchi za jirani.

Naye Mjunbe wa Jumuiya ya wafanyabiashara Honest Kalisti amesema hakuna kurudi nyuma katika mgomo huo, hadi hapo kilio chao kitakaposikilizwa na kutatuliwa huku akisema hili wanalolalamikia Waziri Fedha na Mipango Dk. Mwigulu Nchemba analijua na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa analijua.

Chapisha Maoni

0 Maoni