Mtendaji Mkuu wa Wakala wa nyumba TBA, Daud Kondoro amesema baada ya Rais Samia kuzindua nyumba hizo Machi 23,2022 gharama za nyumba hizo kwa chumba kimoja ni Sh 48,522,913 na nyumba ya vyumba viwili inauzwa Sh 56,893,455.
Maelekezo ya Rais Samia yalikuwa ni kuuzwa kwa nyumba hizo kwa wakazi hao kama Wakazi wanunuzi bila kuzingatia gharama za thamani ya ardhi, maeneo jumuishi kama ngazi, lifti na mandhari ya nje.
Ameeleza kuwa baada ya mapendekezo hayo wakazi hao waliomba kuongezewa muda wa ununuzi wa nyumba hizo pamoja na kupunguziwa gharama hivyo, Rais Samia ameridhia kuwaongezea muda kutoka miaka 15 iliyoelekezwa na serikali awali hadi kuwa miaka 30 ikijumuisha miaka mitano ya kukaa bure.
Kondoro ameeleza kuwa wakazi hao watapaswa kutoa taarifa ya kusudio la kununua nyumba au kutonunua ndani ya siku 14 ili waweze kujibu ambapo mkazi atapaswa kueleza ni utaratibu upi watautumia kulipia nyumba hizo na kwamba wenye uwezo wa kulipa kwa mkupuo wanaruhusiwa.
Kwa upande wao wakazi wanufaika wa mradi huo walionesha kufurahishwa na jambo hilo na kuahidi kufanya malipo hayo kwani suala hilo mwanzoni liligubikwa na utata mkubwa.
Muasisi wa ujenzi huo ni hayati John Pombe Magufuli ambapo April 17,2017 aliweka rasmi jiwe la msingi kuanza kwa ujenzi wa eneo la makazi magomeni kota.
2 Maoni