Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dkt Stergomena Tax amesema zaidi ya raia wa Tanzania 210 wamekwama nchini Sudan kufuatia vita inayoendelea.
Waziri Tax ameyasema hayo Leo Aprili 19 bungeni wakati akitoa tamko la serikali kuhusu vita inayoendelea nchini humo.
“Serikali imeendelea kufanya mawasiliano mara kwa mara na ubalozi wetu ili kujua hali inavyoendelea 171 kati ya hao ni wanafunzi ,wengine ni maafisa wa ubalozi na raia wengine” alisema
TAMKO LA SERIKALI
Katika tamko la nchi kupinga mapigano hayo Waziri Tax amesema Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasikitishwa na hali ya kuzorota kwa amani na usalama inayoendelea.
Tanzania ikiwa kama mjumbe wa baraza la amani na usalama la Umoja wa Afrika inaunga mkono tamko lililotolewa na baraza hilo katika kulaani mapigano hayo na kutoa wito kwa pande zote mbili kusitisha mapigano hayo.
Waziri Tax alisema Tanzania inazitaka pande zote mbili zinazohasimiana kutatua mgogoro kwa njia za amani na usalama huku zikihakikisha mahitaji ya kibinadamu kwa raia na raia wa kigeni.
VITA ILIPOANZA
Tarehe 15 mwezi April nchini Sudan kulizuka mapigano kati ya vikosi vya serikali na vikosi vya msaada katika mji mkuu wa Sudan Khartum na katika maeneo mbalimbali nchini humo.
Mapigano hayo yanatajwa kuchangia kurudisha nyuma huku jitihada mbalimbali zikiendelea katika kutafuta suluhisho baina ya wapiganaji hao.
0 Maoni