Wizara ya Afya imesema kwamba taarifa
za kitabibu zinaonesha kuwa kuanzia tarehe 21 Aprili mwaka huu
Tanzania imedhibiti ugonjwa wa Marburg na hakuna mgonjwa yeyote
mwenye virusi vya ugonjwa ugonjwa huo mkoani Kagera.
Hayo
ameyasema leo Waziri wa Afya Mh. Ummy Mwalimu alipokuwa anaongea na
waandishi wa habari katika ofisi ndogo za wizara hiyo iliyopo Jijini
Dar es Salaam.
“Wagonjwa wawili waliokuwa wamesalia katika
vituo maalum vya matibabu waliruhusiwa kutoka tarehe 20 na 21 Aprili
2023 baada ya kuthibitika kimaabara kuwa hawana tena virusi vya
Marburg,” alisema Waziri Ummy.
Amesema hatua za haraka
zilizochukuliwa na Serikali zilipelekea kuhakikisha ugonjwa huu wa
Marburg hausambai nje ya familia zilizoathirika na kwa watumishi wa
afya waliowahudumia wagonjwa kabla ya kuthibitika uwepo wa ugonjwa
huo.
Pamoja na mambo mengie, Waziri Ummy amesema kuwa tangu uwepo wa ugonjwa huo ulipotangazwa jumla ya watu waliopata maambukizi ni tisa kati ya hao watatu wamepona na wagonjwa sita walipoteza maisha.
Miongoni mwa waliopona ni pamoja na
daktari aliyewahudumia wagonjwa wa mwanzo kabla ya kuthibitika,
miongoni mwa watu waliopoteza maisha ni pamoja na mtumishi mmoja wa
afya na mtoto mwenye umri wa miezi tisa.
Hata hivyo amesema
serikali chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan itaendelea na
ufuatiliaji wa magonjwa ya mlipuko ukiwemo ugonjwa wa Marbug.
“Iwapo hakutatokea mgonjwa mpya mwenye virusi vya Marburg
baada ya siku 42 yaani hadi ifikapo tarehe 31 Mei 2023 ndipo
tutatangaza rasmi kumalizika kwa ugonjwa huu,” amesema Waziri Ummy.
0 Maoni