Amani ni mtaji muhimu wa maendeleo - Askofu Yakobo

 

Wananchi wametakiwa kutambua kuwa amani ni mtaji wa kwanza na muhimu katika kuleta maendeleo ya mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla, kwani huwezesha uzalishaji, ibada za dini kufanyika kwa uhuru na kuimarisha mshikamano wa kijamii.

Wito huo umetolewa na Askofu Mkuu wa Kanisa la Healing Gospel Assemblies of God, John Yakobo, wakati wa ibada ya uwekaji wakfu wa jengo la kanisa hilo lililopo Bomani, Mjini Geita.

Akizungumza katika ibada hiyo, Askofu Yakobo amesema ni muhimu kwa wananchi kutambua na kulinda misingi ya amani kwa kuwa ndiyo msingi wa mafanikio katika nyanja mbalimbali, ikiwemo kuhubiri Injili, maendeleo ya kiuchumi na ustawi wa taifa.

"Amani ndiyo mtaji wa kwanza wa maendeleo. Bila amani hakuna uzalishaji, hakuna ustawi wa jamii wala maendeleo ya taifa. Kila mwananchi ana wajibu wa kuilinda na kuitunza," amesema Askofu Yakobo.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Kanisa la Healing Gospel Assemblies of God, Godlisten Diah, akinukuu maandiko kutoka Kitabu cha Kumbukumbu la Torati sura ya nane mstari wa kwanza, aliwahimiza waumini kuendelea kumtumaini Mungu licha ya changamoto mbalimbali wanazokutana nazo katika maisha.

"Pamoja na magumu na majaribu tunayokutana nayo katika maisha, upendo wa Mungu ni mkuu na wa kudumu. Tunapaswa kuendelea kuwa na imani na kumtegemea Mungu katika kila hatua," amesema Diah.

Baadhi ya waumini walioshiriki ibada hiyo walieleza furaha yao kutokana na kukamilika kwa jengo hilo la kanisa, wakisema litakuwa kitovu muhimu cha kujenga jamii yenye hofu ya Mungu, maadili mema na mshikamano.

Uwekaji wakfu wa jengo hilo umeelezwa kuwa hatua muhimu katika kuimarisha huduma za kiroho katika Mkoa wa Geita na kuchochea maadili yanayolenga kujenga taifa lenye umoja, amani na maendeleo endelevu.



Chapisha Maoni

0 Maoni