Wanaodaia hakuna maendeleo ni wapotoshaji- Kihongosi

 

Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM, Kenani Kihongosi, amesema Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) imeendelea kuleta mageuzi na maendeleo makubwa katika sekta mbalimbali nchini, huku akiwataka wananchi kutambua tofauti ya hali ilivyokuwa miaka ya nyuma na ilivyo sasa.

Kihongosi alitoa kauli hiyo wakati wa hitimisho la ziara ya Mwenezi wa CCM Mkoa wa Kilimanjaro kabla ya kuelekea Mkoa wa Manyara, akisema ni upotoshaji kudai kuwa hakuna maendeleo yaliyofanyika nchini kwani wananchi wanaona na kushuhudia mabadiliko yanayoendelea katika maeneo mbalimbali.

“Ni makosa kusema hakuna maendeleo nchini. Wananchi wanaona tofauti ya Tanzania ya jana na ya leo kupitia miradi na huduma mbalimbali zinazoendelea kutekelezwa na Serikali,” amesema Kihongosi.

Alieleza kuwa kuongoza taifa kubwa kama Tanzania si kazi rahisi kutokana na wingi wa wananchi na mahitaji ya huduma za msingi katika mikoa, wilaya, halmashauri, kata na vijiji, jambo ambalo linahitaji viongozi wenye maono, uthubutu na uwezo wa kufanya maamuzi kwa manufaa ya taifa.

Aidha, Kihongosi alimpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa juhudi zake za kusimamia maendeleo ya nchi, akisema ameendelea kuelekeza nguvu zake katika kuwahudumia wananchi licha ya kukabiliwa na ukosoaji kutoka kwa baadhi ya watu.

“Licha ya changamoto na ukosoaji anaokutana nao, Rais Samia ameendelea kuweka mbele maslahi ya wananchi kwa kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuboresha huduma za kijamii,” amesema.

Amesisitiza kuwa CCM itaendelea kuwaeleza wananchi kuhusu mafanikio ya Serikali na kuhimiza ushiriki wao katika kulinda na kuendeleza maendeleo yaliyopatikana nchini.

Chapisha Maoni

0 Maoni