Profesa Muhongo achaguliwa Baraza la Uongozi la AAS

 

Mwanasayansi bingwa kutoka Tanzania, Sospeter Mwijarubi Muhongo, amechaguliwa kuwa mjumbe wa Baraza la Uongozi la Wasomi wa Sayansi Afrika (AAS) kwa kipindi cha mwaka 2026 hadi 2029.

Katika uchaguzi wa kielektroniki uliofanyika hivi karibuni, Profesa Muhongo alipata kura 168 za ndiyo, kura mbili za hapana na kura 15 za kutokuegemea upande wowote, huku asilimia 74.60 ya wajumbe wenye sifa wakishiriki kupiga kura.

Kwa mujibu wa wasifu wake mfupi, Profesa Muhongo ni msomi mashuhuri wa kiwango cha kimataifa katika sayansi ya dunia na mwanajiolojia aliyesajiliwa barani Ulaya.

Ana shahada ya uzamivu ya Dr.rer.nat. kutoka Chuo Kikuu cha Ufundi cha Berlin nchini Ujerumani.

Mbali na kuwa Waziri wa zamani wa Nishati na Madini wa Tanzania, Profesa Muhongo pia aliwahi kuwa Rais wa Jamii ya Wanajiolojia Afrika na ni mwanachama mwandamizi wa AAS.

Aidha, ametunukiwa hadhi ya Honorary Fellow na Geological Society of London pamoja na Geological Society of America. Pia ni Honorary Research Fellow wa Chinese Academy of Geological Sciences.

Profesa Muhongo pia aliwahi kuwa Mkurugenzi wa kwanza wa Kanda ya Afrika wa Umoja wa Baraza la Kimataifa la Wanasayansi (ICSU).

Chapisha Maoni

0 Maoni