Chama
Cha Mapinduzi (CCM) kupitia kwa Katibu wa Itikadi, Uenezi na Mafunzo
Zanzibar, Khamis Mbeto Khamis, kimewataka viongozi wastaafu, wasomi,
wachambuzi na wanasiasa kulinda umoja na amani ya nchi.
Mbeto
amesema gharama ya kujenga Taifa ni kubwa kuliko hasara ya kulibomoa,
akisisitiza umuhimu wa viongozi na wadau mbalimbali kuwa waandishi na
wasemaji wa heri badala ya kupandikiza chuki na hasama katika
jamii.
Aidha, amekemea tabia iliyoibuka hivi karibuni ya
baadhi ya viongozi wastaafu na wanataaluma wanaotoa kauli kali na za
kuogofya bila kupima athari zake kwa jamii. Amesema maneno
yasiyochujwa yanaweza kuleta madhara makubwa na kusababisha taharuki
isiyo ya lazima.
“Ghasia na machafuko yakizuka hayana macho;
huwadhuru wote matajiri, maskini, viongozi na raia wasio na hatia,”
amesema Mbeto.
Katika hatua nyingine, Mbeto amewasihi wadau
hao kutumia njia za kiungwana na mazungumzo katika kutatua changamoto
za kisiasa na kijamii badala ya kutafuta umaarufu kupitia kauli za
uchochezi.
Pia, ameonya kuwa siasa za kuhubiri chuki na shari
zimechangia kubomoka kwa baadhi ya mataifa barani Afrika kutokana na
vita na umwagaji damu, huku akisisitiza kuwa njia halali ya kupata
madaraka ni kupitia demokrasia ya uchaguzi na si kwa vurugu.

0 Maoni