Waziri wa Fedha azihimiza taasisi za fedha kupunguza riba

 

Na. Benny Mwaipaja- Arusha

Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Balozi Khamis Mussa Omar (MB), ametoa wito kwa Taasisi za Fedha nchini kupunguza riba na gharama nyingine za mikopo ili kuwawezesha wananchi wakiwemo vijana kupata mitaji ya kuwekeza kwenye shughuli zao za kiuchumi.

Mhe. Balozi Omar ametoa rai hiyo wakati akifungua Semina ya Wanahisa wa Benki ya CRDB katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Wanahisa hao, uliobeba kauli mbiu ya "Vijana na Uwekezaji kwenye Hisa" inayofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC).

"Kuna kilio cha wananchi kuhusu kiwango cha riba na ada za huduma za benki, nawahimiza viongozi wa CRDB na taasisi nyingine za fedha hususan benki, kuchukua hatua za kupunguza mzigo wa gharama kwa wateja hasa wanaofungua akaunti na kufanya miamala" alisisitiza Mhe. Balozi Omar.

Aidha, aliipongeza Benki ya CRDB, kwa mafanikio makubwa na kuchangia karibu asilimia 29 ya mikopo kwa sekta binafsi nchini na kufanikiwa kuongeza faida, akitaja faida iliyopata mwaka 2025, iliyofikia shilingi bilioni 725, hatua inayoashiria kufanya vizuri zaidi katika mwaka 2026, ambapo kiwango cha faida cha shilingi trilioni moja kinaweza kufikiwa.

Mhe. Balozi Omar, alisifu pia juhudi za CRDB katika kuendeleza bidhaa za ubunifu za soko la mitaji, ikiwemo ushirikiano katika Samia Infrastructure Bond, uhamasishaji wa hati fungani za kijani, programu za vijana na bidhaa za kifedha zenye msingi wa Sharia, kama Sukuk.

Aliahidi kuwa Serikali kwa upande wake itaendelea kuweka mazingira wezeshi kupitia sera thabiti, maboresho ya mifumo ya kisheria na kuimarisha miundombinu ya kifedha ili kuchochea mchango wa sekta hiyo ya fedha katika kukuza pato la Taifa na kukuza biashara na uwekezaji.

Mhe. Balozi Omar, aliwataka vijana kujenga utamaduni wa kuwekeza katika hisa na bidhaa za masoko ya mitaji ili kujihakikishia mustakabali wa kifedha na kuchangia ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Kwa Upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dkt. Abdul Majid Nsekela, alisema benki yake imeweka mikakati maalumu ya kuwajumuisha vijana kumiliki shughuli za kiuchumi kupitia bidhaa na huduma za kifedha ikiwemo Youth Banking, Junior Jumbo, Teens Account, Scholar Account na Boom Advance.

Akizungumzia kuhusu mafanikio ya CRDB, alisema kuwa benki hiyo imeendelea kukua kwa kasi: mali za benki zilifikia TZS trilioni 23.9 mwanzoni mwa 2026, amana za wateja zimefikia sh. trilioni 16.3 na mikopo iliyotolewa imefikia sh. trilioni 14.7 huku faida ya benki ilifikia sh. bilioni 725 mwaka 2025, ongezeko la zaidi ya asilimia 1,000 katika miaka ya hivi karibuni.

Aliongeza kuwa CRDB imeongeza jitihada za kibunifu za benki, zikiwamo ushirikiano kwenye Samia Infrastructure Bond, uhamasishaji wa hati fungani za kijani, bidhaa za kifedha za misingi ya Sharia (Sukuk), na programu maalumu kwa vijana.

Aidha, alitoa shukrani kwa Serikali kwa kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji, na taasisi za udhibiti kama Benki Kuu ya Tanzania, Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) na CMSA kwa michango yao katika kukuza masoko ya mitaji.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB, Prof. Neema Mori, alibainisha kuwa idadi ya wanahisa wa CRDB imeongezeka kwa kasi kutoka 30,141 mwaka 2021 hadi 89,194 hadi Machi 2026, kiwa ni sawa na ongezeko la asilimia 195.92.

"Hali hii inaonesha kuwa kuna hamasa kubwa ya umma, hasa vijana, katika kununua hisa za benki. Alielezea furaha yake kuona kuwa CRDB imegeuka kutoka kuwa "household brand" hadi "investors brand" yenye mvuto kwa wawekezaji wadogo na wakubwa" alisema Prof. Mori.

Semina hiyo imewashirikisha baadhi ya Wakuu wa mikoa, Mkuu wa Wilaya ya Arusha, wajumbe wa Bodi, Menejimenti ya CRDB, wanahisa na waandishi wa habari huku Mada zinazojadiliwa ni kuhamasisha uwekezaji wa vijana, utoaji gawio, na mbinu za kukuza ushiriki wa wananchi katika masoko ya mitaji.




Chapisha Maoni

0 Maoni