Vyama 12 vya siasa nchini vimejitokeza kwa pamoja kupongeza ripoti ya Tume ya Kuchunguza Matukio ya Uvunjifu wa Amani wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, vikisema imegusa kwa kina changamoto zilizojitokeza na kutoa mapendekezo yenye mwelekeo wa kulinda amani na mshikamano wa kitaifa. Aidha, vyama hivyo vimetaka kuharakishwa kwa mchakato wa maridhiano pamoja na kupatikana kwa Katiba mpya, kama ilivyopendekezwa na tume hiyo.

Akizungumza leo Aprili 26, 2026 jijini Dar es Salaam mbele ya waandishi wa habari, wawakilishi wa vyama hivyo walisema pendekezo la kuanza mchakato wa Katiba mpya kabla ya mwaka 2028 linapaswa kupewa uzito wa kipekee. Walisisitiza kuwa hatua hiyo inaweza kuwa suluhu ya kudumu kwa changamoto za kisiasa, kijamii na kiuchumi zinazoikabili nchi kwa sasa.

Vyama vilivyoshiriki katika tamko hilo la pamoja ni DP, NRA, NLD, AAFP, ADA-TADEA, Demokrasia Makini, UPDP, UDP, SAU, UMD, TLP na CCK, vikionyesha mshikamano wa nadra katika masuala ya msingi ya kitaifa. Kauli yao ya pamoja imeelezwa kuwa ishara ya utayari wa kushirikiana kwa lengo la kuimarisha demokrasia na utawala bora nchini.

Katika tamko hilo, vyama hivyo vimesisitiza kuwa viko tayari kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa mapendekezo yote yaliyotolewa na tume, wakieleza kuwa ushirikiano huo ni muhimu katika kudumisha amani, utulivu na kuondoa migogoro ya kisiasa inayoweza kujitokeza siku zijazo.

Akizungumza kwa niaba ya vyama hivyo, Hassan Doyo, aliyekuwa mgombea urais kupitia NLD katika uchaguzi mkuu wa 2025, alisema kupatikana kwa Katiba mpya hakutaishia kutatua changamoto za kisiasa pekee, bali pia kutasaidia kulijenga upya Taifa na kurejesha imani miongoni mwa wananchi. “Kupitia maridhiano na Katiba mpya, nchi itaendelea kuwa na amani na utulivu wa kudumu,” alisisitiza Doyo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa jukwaa hilo, Abdul Muya, alimpongeza mwenyekiti wa tume hiyo, Mohamed Othman Chande, kwa kazi kubwa iliyofanywa, akieleza kuwa ripoti hiyo imeweka msingi imara wa majadiliano ya kitaifa. Pia alitoa wito wa kuitishwa kwa Baraza la Vyama vya Siasa ili kujadili kwa kina mapendekezo yote yaliyomo kwenye ripoti hiyo na kuweka mkakati wa utekelezaji wake.

Muya aliongeza kuwa ni muhimu kwa vyombo vya dola kuchukua hatua stahiki dhidi ya vichocheo vilivyotajwa kwenye ripoti hiyo kama sababu ya ghasia za Oktoba 2025, ili kuzuia matukio kama hayo kujirudia. Alisisitiza kuwa uwajibikaji ni sehemu muhimu ya mchakato wa maridhiano ya kweli.

Wakati Rais Samia Suluhu Hassan, alipokuwa akipokea ripoti hiyo, alieleza dhamira ya Serikali yake kuhakikisha upatikanaji wa Katiba mpya katika kipindi chake cha pili cha uongozi. Pia alitangaza kuundwa kwa Tume ya Maridhiano katika siku za karibuni, itakayokuwa na jukumu la kuratibu na kusimamia mchakato mzima wa maridhiano nchini.


#UmojaWetuNdiyoNguvuYetu
#turidhiane