Dkt. Mchunguzi aipongeza Tume ya Chande kwa kazi nzuri ya siku 153

 

Mtaalamu wa maridhiano na utatuzi wa migogoro, Dkt. Dennis Mchunguzi, ameisifu Tume ya Uchunguzi iliyoongozwa na Mohamed Othman Chande kwa kutekeleza jukumu lake kwa mafanikio ndani ya siku 153, akibainisha kuwa kazi hiyo ilihitaji kiwango cha juu cha umakini, weledi na uzalendo.

Pia alimpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa uamuzi wa kuunda tume hiyo, akieleza kuwa hatua hiyo inaonesha nia ya dhati ya Serikali katika kutafuta ukweli na kuimarisha misingi ya haki pamoja na amani nchini.

Akizungumza baada ya kuisoma ripoti hiyo, Dkt. Mchunguzi alisema imeandaliwa kwa ustadi mkubwa wa kitaaluma, ikizingatia viwango vinavyotakiwa na kutekeleza kikamilifu hadidu za rejea zilizopewa tume hiyo.

Hata hivyo, alieleza masikitiko yake kufuatia madhara yaliyosababishwa na vurugu za Oktoba 29, zikiwemo vifo vya watu, majeruhi pamoja na uharibifu wa mali, akisisitiza kuwa matukio hayo yameacha athari kubwa kwa jamii na taifa kwa ujumla.

Alijiunga na Rais Samia kutoa pole kwa familia zilizopoteza wapendwa wao na wale walioathirika kwa namna mbalimbali, akihimiza mshikamano wa kitaifa katika kipindi hiki.

Aidha, alibainisha kuwa ripoti hiyo ni nyenzo muhimu katika kujenga msingi imara wa haki, uwajibikaji na maridhiano ya kweli, ambayo ni muhimu kwa mustakabali wa nchi.

Alisisitiza pia umuhimu wa kudumisha umoja wa kitaifa na kuchukua tahadhari dhidi ya vitendo au mienendo inayoweza kuhatarisha maendeleo ya taifa.

#UmojaWetuNdiyoNguvuYetu

#turidhiane


Chapisha Maoni

0 Maoni