Jeshi la Polisi limesema kuwa taifa limeamka salama
na hali ya utulivu imetawala katika maeneo mbalimbali ya nchi, hali inayotajwa
kuwa matokeo ya ushirikiano unaotolewa na wananchi kwa vyombo vya ulinzi na
usalama.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo iliyotolewa leo na
Msemaji Mkuu wa Polisi David Misime, Tanzania imeanza siku ikiwa shwari huku
utekelezaji wa majukumu ya ulinzi ukiendelea kama kawaida.
Katika maelezo yao, Jeshi la Polisi limebainisha
kuwa linaendelea kufanya kazi kwa karibu na vyombo vingine vya ulinzi katika
kulinda maisha, mali na usalama wa raia.
Limesisitiza umuhimu wa wananchi kuendeleza desturi
ya kufuata sheria na kuzingatia kanuni za kiusalama, ambazo zinapaswa kuanzia
ngazi ya mtu mmoja mmoja na kwa jamii nzima kwa ujumla.
Taarifa hiyo imeelekeza pia umuhimu wa kukataa na
kupuuza taarifa zinazotumiwa kuchochea chuki, uzushi, uongo au vitendo
vinavyoweza kuhatarisha utulivu wa nchi.
Wananchi wametakiwa kufuta ujumbe wa aina hiyo
endapo watakutana nao mtandaoni na kutowapa nafasi watu wanaojitokeza kwa
mashinikizo ya kuhamasisha vurugu au uvunjifu wa sheria.
Jeshi la Polisi limehitimisha kwa kuwataka wananchi
kuendelea na shughuli zao halali bila hofu, likisisitiza kuwa nchi inaendelea
kuwa salama kutokana na ushirikiano kati ya wananchi na vyombo vya ulinzi na
usalama.
Limewatia moyo Watanzania kutanguliza uwajibikaji na
kuendelea kulinda amani ambayo imekuwa msingi wa maisha na maendeleo ya taifa.

0 Maoni