SPIKA
wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mussa Azzan Zungu, ametangaza
msiba mzito wa Mbunge wa Peramiho, Jenista Joakim Mhagama, aliyefariki dunia
leo Alhamisi, Desemba 11, 2025, jijini Dodoma.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa kifo hicho kimelitikisa Bunge
pamoja na wananchi wa Jimbo la Peramiho ambako marehemu alikuwa akiendelea
kuhudumu.
Kupitia taarifa yake, Spika Zungu ameonesha
masikitiko makubwa na kutoa pole kwa wabunge, familia ya marehemu, ndugu, jamaa
pamoja na wakazi wa Peramiho.
Amesema kuwa taifa limempoteza kiongozi aliyekuwa na
mchango mkubwa katika uongozi na utumishi wa umma, huku akiwataka wote
walioguswa na msiba huo kuwa na subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu.
Jenista Mhagama, ambaye alizaliwa Juni 23, 1967,
amewahi kushika nafasi mbalimbali serikalini na bungeni, na alikuwa miongoni
mwa viongozi waliotajwa kwa utendaji na ushiriki mkubwa katika masuala ya
kitaifa.
Kwa mujibu wa taarifa ya Bunge, taratibu za mazishi
zinaendelea kuratibiwa kwa ushirikiano na familia ya marehemu, na maelezo ya
ziada yataendelea kutolewa kadiri maandalizi yatakavyokamilika.


0 Maoni