Tunapouaga rasmi mwaka 2025, Mwenyekiti wa Tanzania
Bloggers Network (TBN), Beda Msimbe, amewapongeza Watanzania wote kwa kumaliza
mwaka huo kwa uthabiti, moyo wa kizalendo na mshikamano, akieleza kuwa umekuwa
mwaka wenye matukio mengi ya kihistoria kwa Taifa.
Akitoa salamu za mwaka mpya kwa niaba ya wanachama wote wa
TBN, Msimbe amewashukuru wasomaji na wadau mbalimbali kwa kuendelea kufuatilia
habari, uchambuzi na taarifa kupitia majukwaa ya kidijitali ya mtandao huo,
akisisitiza kuwa mchango wao umekuwa nguzo muhimu katika kukuza tasnia ya
habari za mtandaoni nchini.
“Kupitia ushiriki wenu, TBN imeendelea kuwa sauti ya
wananchi na jukwaa huru la mijadala yenye tija kwa maendeleo ya Taifa,” amesema
Msimbe.
Mageuzi Makubwa 2026
Akizungumzia matarajio ya Mwaka Mpya 2026, Mwenyekiti huyo
amesema TBN imejipanga kuleta mageuzi makubwa yatakayolenga kuboresha ubora wa
maudhui, kuimarisha matumizi ya teknolojia ya kisasa, pamoja na kuwasilisha
habari za kina zitakazosaidia wananchi kufanya maamuzi sahihi.
Ameeleza kuwa wanachama wa TBN wataendelea kuwa daraja
imara kati ya serikali na wananchi kwa kuhakikisha habari sahihi, za kuaminika
na kwa wakati zinafika kwa kila Mtanzania, mijini na vijijini.
Wito wa Amani na Umoja
Katika salamu zake za Mwaka Mpya, Msimbe ametoa wito kwa
Watanzania kuendelea kudumisha amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa,
akisisitiza umuhimu wa kuepuka migawanyiko na vurugu zisizo na tija.
“Huu ni wakati wa kuungana kwa nguvu moja ili kutekeleza
Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050. Lengo ni kuhakikisha kila Mtanzania anafaidika
na maendeleo ya kweli na anapata sehemu yake ya ‘keki ya taifa’,” amesema.
Ujumbe wa Heri ya Mwaka Mpya
Akihitimisha ujumbe wake, Mwenyekiti wa TBN amewaombea
Watanzania mwaka 2026 uwe mwaka wa neema, baraka na mafanikio tele katika kazi
na shughuli zao za kila siku.
“Heri ya Mwaka Mpya 2026 kwa Watanzania wote,” amehitimisha
Msimbe.

0 Maoni