Bajeti ya Elimu Zanzibar kupanda hadi Trilioni 1

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi amesema kuwa Serikali inalenga kuimarisha bajeti ya sekta ya elimu kutoka shilingi Bilioni 864 hadi kufikia shilingi Trilioni 1.

Amesema Serikali itaendelea kuimarisha mazingira bora ya ufundishaji, maslahi na posho za walimu pamoja na ujenzi wa miundombinu ya elimu ili kuifanya Zanzibar kuwa na elimu bora.

Rais Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo tarehe 05 Disemba 2025 katika ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa 13 wa Jumuiya ya Walimu Wakuu wa Skuli za Sekondari za Zanzibar (JUWASEZA), uliofanyika katika ukumbi wa Skuli ya Fidel Castro sambamba na ufunguzi wa Dakhalia mpya ya wanafunzi wa kike wa skuli hiyo iliyopo Mkoa wa Kusini Pemba.

Akizungumzia ujenzi wa Dakhalia, amesema ni mkakati maalum wa Serikali wenye lengo la kuimarisha sekta ya elimu nchini. Ameeleza kuwa Serikali itaendelea kujenga Dakhalia katika kila wilaya ili kufikia idadi ya wanafunzi 10,000 wanaosoma katika skuli za Dakhalia ifikapo mwaka 2030.

Dkt. Mwinyi ametoa rai kwa walimu wakuu kuwa wasimamizi madhubuti wa miundombinu ya elimu, ufaulu wa wanafunzi na rasilimali za umma katika maeneo waliyopewa dhamana na kuahidi kutenga mafungu maalum ya fedha kwa ajili ya ukarabati wa miundimbinu ya elimu pale inapohitajika.

Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amewahakikisha walimu kuwa Serikali ipo tayari kutatua changamoto zinazowakabili ili kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao kwa ufanisi.

Akihitimisha hotuba yake, Rais Dkt. Mwinyi ameahidi kuyaangalia upya maslahi ya walimu wastaafu pamoja na watumishi wengine wa sekta ya umma kwa lengo la kuimarisha maisha yao, ikiwemo upatikanaji wa nyumba bora za kuishi, pensheni na posho.

Naye Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Mhe. Lela Mohamed Mussa, amesema mageuzi makubwa yanayoendelea katika sekta ya elimu yametokana na imani, maono na juhudi kubwa zinazochukuliwa na Rais Dkt. Mwinyi katika kuleta mageuzi na maendeleo ya sekta hiyo.

Amebainisha kuwa uwekezaji mkubwa unaofanywa katika sekta hiyo, hususan katika miundombinu ya elimu, umeongeza ari ya walimu kutekeleza majukumu yao kwa weledi na ufanisi.

Akitoa taarifa ya kitaalamu ya ujenzi wa Dakhalia ya wanafunzi wa kike, Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, Khamis Abdallah Said, amesema ujenzi huo umegharimu shilingi Bilioni 1.5 na una uwezo wa kuchukua wanafunzi 288 kwa wastani wa wanafunzi 28 kwa kila darasa. Aidha, amesema Wizara ya Elimu inakusudia kujenga Dakhalia nyingine 16 Unguja na Pemba katika mwaka wa fedha wa 2025–2026.

Mradi wa Dakhalia ya wanafunzi wa kike wa Skuli ya Fidel Castro unakuwa mradi wa kwanza kufunguliwa na Rais Dkt. Mwinyi kisiwani Pemba tangu alipochaguliwa tena kuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kuiongoza tena Zanzibar kwa kipindi cha pili cha Awamu ya Nane.



Chapisha Maoni

0 Maoni