Zikiwa zimebaki siku chache kabla ya Uchaguzi Mkuu
wa Oktoba 29, 2025, viongozi wa dini nchini kote wameungana kutoa wito wa
kitaifa, wakisisitiza Watanzania wote kudumisha amani, umoja, na mshikamano, wakitaja
amani kuwa msingi wa maendeleo ya Taifa.
Wito huu wa pamoja unasisitiza kuwa Tanzania lazima
iendelee kuwa “Kisiwa cha Amani,” hadhi ambayo imechangia mafanikio makubwa ya
kiuchumi, ikiwemo ongezeko la watalii kutoka 620,867 mwaka 2020 hadi $1,924,240$
mwaka 2024, na kupanda kwa mapato ya utalii kutoka USD milioni 700 hadi USD
bilioni 3.3.
Msisitizo Kutoka Kanda Mbalimbali
Wito wa Tabora: Amani ni Dini
Kutoka Tabora, Askofu Dkt. Elias Chakupewa wa Kanisa
la Anglikana na Mwenyekiti wa Kamati ya Dini na Amani Mkoa, aliwakumbusha
wananchi kuwa hakuna dini yoyote duniani inayofundisha chuki au vurugu.
“Msingi wa kila dini ni amani. Bila utulivu hapa
duniani haiwezekani kuifikia Mbingu. Vijana tunalo jukumu la pekee la kudumisha
amani hasa kuelekea Uchaguzi Mkuu,” alisema Askofu Chakupewa.
Alionya kuwa amani haiwezi kununuliwa kwa fedha wala
kubadilishwa na rasilimali yoyote, akisisitiza viongozi wa dini lazima
waendelee kuonya wale wachache wanaotaka kuvuruga utulivu wa Taifa.
Wito wa Kaskazini: Kampeni za Kistaarabu
Katika Kanda ya Kaskazini, viongozi walitoa wito
Moshi, Kilimanjaro, wenye kaulimbiu: “Kupiga Kura ni Haki Yetu, Amani ya Taifa
Letu ni Wajibu Wetu.” Walisisitiza kuwa kampeni za kisiasa ziwe za kistaarabu,
zenye hoja, na si matusi.
Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Godfrey Mnzava, alisema
Serikali itahakikisha uchaguzi unafanyika kwa utulivu. "Hakuna maendeleo
bila amani. Watanzania tunatakiwa kuwa mfano wa demokrasia ya kweli barani
Afrika,” alisema Mnzava.
Wito wa Dar es Salaam: Kiongozi wa Dini Awe Sauti ya
Upendo
Viongozi wa dini wa Dar es Salaam nao wametoa onyo
kali. Sheikh Alhad Mussa Salum, akizungumza na waumini, alisisitiza jukumu la
kiongozi wa kiroho:“Kiongozi wa dini anapaswa kuwa sauti ya upendo, si chuki,
kwa sababu anayetaka damu imwagike ni shetani pekee.”
Amani ni Wajibu wa Kila MmojaViongozi hao wa dini
wametoa rai kwa Watanzania wote bila kujali imani, kabila au chama, kuendelea
kuwa walinzi wa amani wakati wote wa Uchaguzi na hata baada yake.
“Tanzania ni kisiwa cha amani, na sisi sote tumepewa
jukumu la kuilinda. Amani yetu si bidhaa ya madukani, ni tunu ya Mungu.
Tukubali kuitunza kwa vizazi vijavyo,” walisisitiza.

0 Maoni