Kuwaita Wastaafu: Kurejesha uzoefu, si njama ya kisiasa

 

Katikati ya mijadala ya kisiasa inayoendelea kuelekea uchaguzi, hatua ya Serikali ya kuwaita baadhi ya maafisa wa Jeshi la Polisi walio staafu kurejea kazini kwa mkataba imejikuta ikivutwa kwenye dimbwi la siasa na kupotosha. Hata hivyo, wachambuzi wa masuala ya usalama wanasisitiza kuwa utaratibu huu si jambo geni na unalenga kujaza ombwe la utaalamu na uzoefu unaohitajika katika kipindi hiki nyeti.

Kiapo cha Utii Kinabaki Hai

Kwa mujibu wa wataalamu wa menejimenti ya vikosi vya usalama, madai kwamba kurejeshwa kazini kwa wastaafu kunaashiria njama au udhaifu wa kiusalama hayana msingi wa kiutawala wala kisheria. Kimsingi, askari wa Tanzania huchukua kiapo cha utii na uaminifu kwa Taifa ambacho, kisheria, kinabaki hai hata baada ya kustaafu.

Kiapo hiki huruhusu askari hao kuitwa tena kazini kulingana na mahitaji maalum ya kitaifa ili kutoa nguvu kazi au uzoefu wa ziada. Hatua hii huonekana katika nchi nyingi duniani, hasa katika taasisi zinazohitaji utaalamu usiopatikana kwa urahisi, kama vile jeshi na polisi. 

Uzoefu Muhimu Katika Ulinzi wa Uchaguzi

Taarifa za ndani ya Jeshi la Polisi zinaeleza kuwa kuitwa kwa askari hawa wastaafu, ambao wengi wao wana uzoefu mkubwa katika kulinda usalama na amani wakati wa chaguzi zilizopita, ni utaratibu wa kujenga uwezo wa kiutendaji.

Jukumu kuu la Jeshi la Polisi wakati wa uchaguzi ni kulinda raia na mali zao, kulinda masanduku ya kura, na kuhakikisha amani inakuwepo. Kwa hiyo, kiongezeko chochote cha nguvu kazi ya ulinzi, hasa kutoka kwa watu wenye uzoefu wa muda mrefu, kinalenga kuimarisha amani hiyo na utulivu wa mchakato, na si kuuvuruga.

Kudhibiti Siasa za Upotoshaji

Jaribio la kutafsiri utaratibu huu wa kawaida wa kiutawala kuajiri wataalamu wastaafu kwa mkataba kutokana na uhitaji kama propaganda ya chuki au hofu ni hatua ya kisiasa inayolenga kutafuta kasoro hata katika hatua za msingi za ulinzi wa Taifa.

Ukweli wa amani na utulivu wa Watanzania haubadiliki kwa sababu ya taarifa za kupotosha. Tanzania ina mfumo wa ulinzi unaoheshimu sheria. Kufanya siasa kwa kutumia mbinu za kuchochea hofu kuhusu usalama wa uchaguzi kunakumbana na ukweli wa utaratibu uliowekwa kisheria wa Serikali wa kutumia uzoefu wa watumishi wake wa zamani. Watanzania wengi wanajua thamani ya amani na hawatadanganywa kwa urahisi.

Chapisha Maoni

0 Maoni