CCM ikae pembeni vilio vya maisha magumu ni vingi - Mwalim

 

Mgombea wa urais kwa tiketi ya Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMMA), Salum Mwalim, amesema wananchi wa maeneo mbalimbali ya vijijini na mijini wamechoshwa na hali ya maisha magumu, ukosefu wa ajira na ubovu wa miundombinu, wakitaka mabadiliko ya kweli ya uongozi.

Akihutubia mkutano wa kampeni uliofanyika leo katika viwanja vya Mbagala Zakhem, jijini Dar es Salaam, Mwalim amesema kila anakopita kwenye kampeni anakutana na kilio cha wananchi wanaolalamikia umaskini uliokithiri.

“Kila ninapopita, wananchi wananililia kuhusu maisha magumu, hali mbaya ya barabara, huduma duni za afya na elimu. Wengi wao, hasa vijana, wanasema wamechoka na mwaka huu wanataka msela wao akalie kiti cha Rais,” amesema Mwalim.

Mwalim amesema taifa linahitaji mabadiliko ya kweli, akisisitiza kuwa ni wakati wa kuipa nafasi CHAUMMA kuongoza nchi, huku akitoa wito kwa Chama cha Mapinduzi (CCM) "kukaa pembeni" kupisha mabadiliko ya kiutawala.

“Tumechoka na maisha magumu. Tumechoka na uonevu. Tunahitaji mabadiliko ya kweli. CCM ikae pembeni,” amesema.

Mwalim ambaye ameendelea na ziara ya kampeni katika mikoa mbalimbali, amesema CHAUMMA iko tayari kuleta mabadiliko ya kiuchumi na kijamii kwa Watanzania wote, hasa makundi ya vijana na wanawake ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakisahaulika.

Kauli zake zimekuja wakati vyama vya siasa nchini vikiendelea na kampeni kuelekea Uchaguzi Mkuu, huku wananchi wakifuatilia kwa karibu mijadala ya kisera kutoka kwa wagombea mbalimbali.

Chapisha Maoni

0 Maoni