Wadaiwa wa utekaji wauawa na Polisi Mbeya

 

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limewaua watu wawili wanaodaiwa kuwa sehemu ya genge lililomhusisha na utekaji na mauaji ya mwanafunzi wa mwaka wa kwanza wa Chuo Kikuu cha Mzumbe tawi la Mbeya, marehemu Shyrose Michael Mabula (21).

Tukio hilo limekuja wiki mbili baada ya mwili wa marehemu Shyrose kupatikana Septemba 16, 2025 majira ya saa 5:00 usiku katika Mtaa wa Morovian, Kata ya Isyesye jijini Mbeya, ukiwa umechomwa moto. Taarifa za awali zilieleza kuwa marehemu alikuwa ametekwa na watu wasiojulikana Septemba 14, 2025.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Benjamin Kuzaga uchunguzi wa awali ulioanzishwa mara baada ya tukio hilo uliwawezesha maofisa wa upelelezi kumtia nguvuni Marwa Nyahega John (25), mkazi wa Uzunguni “A” Mbeya, aliyekiri kuhusika kwenye utekaji huo pamoja na wenzake wawili Edward Christopher Kayuni na Websta William Mwantebele.

Kamanda Kuzaga alisema kuwa watuhumiwa hao walimteka Shyrose kwa lengo la kumtumia kama chambo cha kupata kiasi kikubwa cha fedha kutoka kwa baba yake mzazi, Dkt. Michael Mabula. Baada ya kushindwa kufanikisha mpango huo, walimuua kwa kumlazimisha kunywa sumu ya kuulia magugu aina ya Round Up, kisha walimnyonga na baadaye kuchoma mwili wake ili kuficha ushahidi.

Mauaji Wakiwa Mikononi mwa Polisi

Taarifa ya Polisi inaeleza kuwa tarehe 25 Septemba, 2025, mtuhumiwa Websta William Mwantebele (27), ambaye ni mlinzi, alikamatwa na kuhojiwa, ambapo alikiri kushiriki katika utekaji na kuua binti huyo. Pia alieleza kuwa walikuwa wamepanga kukutana na wenzake waliobaki katika eneo la machimbo, Kijiji cha Chalangwa, Wilaya ya Chunya.

Mnamo Septemba 27, 2025, Mwantebele aliwaongoza askari hadi eneo hilo kwa ajili ya kuwaonyesha wenzake. Askari walijipanga na kuweka mtego, ambapo muda mfupi baadaye alifika mtu aliyedaiwa kuwa ni Edward Christopher Kayuni.

Alipoelezwa kuwa anakamatwa, alitoa kisu ghafla na kujaribu kuwashambulia askari. Hata baada ya onyo la mara kadhaa na risasi za hewani, mtuhumiwa alikaidi na ndipo alipopigwa risasi mguuni na kuanguka.

Wakati purukushani hiyo ikiendelea, mtuhumiwa Websta William Mwantebele naye alijaribu kukimbia kuelekea kichakani, lakini alipigwa risasi mguuni na mgongoni baada ya kushindwa kusimama licha ya onyo. Watuhumiwa wote wawili walikimbizwa katika Hospitali ya Wilaya ya Chunya, lakini walithibitishwa kufariki dunia mara baada ya kufikishwa hospitalini.

Ushirikiano na Mganga wa Jadi

Katika hatua nyingine ya uchunguzi, mtuhumiwa Marwa Nyahega John alieleza kuwa baada ya mauaji, alimkata marehemu kidole cha mkono wa kushoto na pamoja na nguo zake za ndani, alizipeleka kwa mganga wa jadi maeneo ya Isyesye kwa ajili ya kufanya “zindiko” ili wasibainike na kukamatwa na Polisi.

Akiwa njiani kuwaongoza askari hadi kwa mganga huyo, Marwa aliruka ghafla kutoka ndani ya gari la Polisi na kujeruhiwa vibaya kichwani. Alikimbizwa Hospitali ya Rufaa Kanda ya Mbeya ambako alithibitishwa kufariki dunia.

Katika upekuzi uliofanywa kwenye maficho ya watuhumiwa, Polisi walikuta pingili mbili za vidole, vitambulisho bandia viwili vya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) vilivyo na majina na picha za watuhumiwa hao, pamoja na simu mbili zilizokuwa na picha na taarifa mbalimbali zinazoonyesha mawasiliano na ushahidi wa utekaji.

Jeshi la Polisi Latoa Rai

Akizungumza na waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Kuzaga alitoa wito kwa vijana waliopitia mafunzo ya kijeshi au ya kiusalama kutumia ujuzi huo kwa mujibu wa sheria na si kwa kutenda vitendo vya kihalifu.

Aidha, alitoa tahadhari kwa wananchi kuacha tamaa ya kutaka utajiri wa haraka kwa njia za uhalifu, akisisitiza kuwa sheria haitamwacha yeyote atakayehusika na vitendo vya utekaji, mauaji au ushirikiano na magenge ya kihalifu.

"Tunaendelea na msako wa kuwatafuta washirika wengine wa genge hili, ikiwemo mganga wa jadi aliyepokea viungo vya marehemu. Hatutapumzika mpaka wote waliohusika wakamatwe na kufikishwa mbele ya sheria," alisema Kamanda Kuzaga huyo.



Chapisha Maoni

0 Maoni