Dkt. Samia: Tanga kaeni mkao wa kula

 

Mgombea urais kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amewataka wakazi wa Mkoa wa Tanga kukaa 'mkao wa kula' kutokana na mipango ya miradi ya maendeleo itakayoufungua mkoa huo.

Amesema akipewa tena ridhaa ya kuiongoza serikali ijayo ya Tanzania, atairejesha Tanga ya viwanda kwani viwanda ni moja ya kipaumbele cha serikali katika miaka mitano ijayo.

Dkt. Samia ametoa kauli hiyo leo Jumatatu Septemba 29, 2025 kwenye Viwanja vya Usagara jijini Tanga alipohutubia maelfu ya wananchi katika mkutano wa kampeni.

"Wana Tanga mkae mkao wa kula. Tunataka kuirejesha ile Tanga ya viwanda," alisema.

Amesema tayari Tanga imekuwa na mafanikio na maendeleo makubwa kutokana na maboresho ya Bandari ya Tanga ambayo itakuwa na bohari ya mafuta na gesi.

Kutokana na maboresho hayo, bandari hiyo itaongeza ajira 2,100 kwa wana Tanga na kunyanyua uchumi wa wananchi wake.

Aidha, amesema Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP) umefikia asilimia 84 na umetoa ajira 1,300 kwa wakazi wa Chongoleani na jumla ya ajira 2,000 ndani ya Tanga.

Akizungumza mambo mazuri yajayo kwa wana Tanga, Dkt. Samia amesema serikali itajenga reli ya Tanga - Arusha - Musoma ya kilometa 1,108 ambayo itaongeza fursa za ajira na kukuza uchumi.

Amesema Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) kwa kushirikiana na Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) watajenga Barabara ya Handeni - Singida.

Ameutaja mkakati mwingine kuwa ni kuipanua Barabara ya Dar es Salaam - Chalinze - Segera kwa nia ya kupunguza msongamano wakati Mkoa wa Tanga ukifunguka kiuchumi.

Katika kuirejesha Tanga ya viwanda, Dkt. Samia amesema kutajengwa Kiwanda cha Chai Korogwe, huku Kiwanda cha Foma kikiwa kimeshafufuliwa,na Kiwanda cha Saruji Tanga kimepanuliwa na kuongeza uzalishaji na kunajengwa kiwanda cha kuunganisha magari ya kubeba wagonjwa(ambulance).

"Haya yote yanaongeza uwekezaji, hivyo maeneo yaliyokamatwa na watu ambayo hayajaendelezwa yatwaliwe na kupewa wawekezaji," amesema Dkt. Samia.

Amebainisha kuwa kutajengwa viwanda viwili vya sukari, kimoja katika Bonde la Pangani kwa sukari ya majumbani na kingine Tanga kwa sukari ya viwandani.

Pia katika bonde hilo kutakuwa na skimu ya umwagiliaji itakayotoa ajira 20,000 itakayojengwa kwa gharama ya Shilingi bilioni 87.

Amewaahidi machinga kuwa serikali yake ijayo itawajengea soko lenye uwezo wa kuwahudumia wafanyabiashara 1,400 kwa gharama ya Shilingi bilioni 1.9,

pamoja na ujenzi wa kiwanda cha dawa na vifaa tiba.

Akiwa Pangani, ameahidi kukamilisha Daraja la Pangani na Barabara ya Tanga - Pangani - Makurunge, pamoja na ujenzi wa soko la kimataifa la samaki Kipumbwi.

Akiwa Muheza, mbali ya kuahidi kujenga na kukamilisha barabara za Muheza - Pangani kilometa 45 na Muheza - Amani kilometa 40,mgombea huyo wa Urais wa CCM ameahidi serikali ijayo itajenga kongani za viwanda vya matunda na viungo.

Aboubakary Liongo - Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano Idara ya Itikadi, Uenezi na Mafunzo CCM

Chapisha Maoni

0 Maoni