Tanzania yaipongeza China kwa miaka 76 ya mafanikio

  

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetoa salamu za pongezi kwa Jamhuri ya Watu wa China (PRC) kwa kuadhimisha miaka 76 tangu kuanzishwa kwa taifa hilo, ambalo kwa sasa lina nafasi ya pili kwa ukubwa wa uchumi duniani. 

Salamu hizo ziliwasilishwa kwa niaba ya Serikali ya Tanzania na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Balozi Mahmoud Thabit Kombo, katika hafla maalumu ya maadhimisho iliyofanyika Septemba 29, 2025 katika makazi ya Balozi wa China jijini Dar es Salaam. 

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Waziri Kombo aliipongeza China kwa hatua kubwa ilizopiga katika nyanja za maendeleo ya kiuchumi, sayansi na teknolojia ndani ya kipindi cha miaka 76 tangu kuanzishwa kwake, akieleza kuwa taifa hilo ni mfano wa kuigwa duniani na mshirika muhimu kwa maendeleo ya Afrika, hasa Tanzania. 

“Uhusiano kati ya Tanzania na China ni wa kihistoria, uliosimikwa katika misingi ya urafiki, uwazi, usawa na kuheshimiana. Tunafarijika kuona uhusiano huu ukizidi kuimarika kupitia ushirikiano katika maeneo mbalimbali kama biashara, uwekezaji, elimu, afya, kilimo, utalii na miundombinu,” alisema Mhe. Kombo. 

Aidha, Waziri Kombo alieleza dhamira ya Tanzania ya kuendelea kushirikiana kwa karibu zaidi na China katika kusaka fursa mpya za maendeleo na kuhakikisha misingi iliyoweka uhusiano huo inadumishwa, akibainisha kuwa msingi huo ndiyo dira ya uhusiano imara uliodumu kwa karibu miongo sita. 

Kwa upande wake, Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania, Mhe. Chen Mingjian, alisema licha ya changamoto za kisiasa na kiuchumi zinazolikumba dunia kwa sasa, China imeendelea kusimama imara katika kulinda ustawi wa wananchi wake na kuchangia maendeleo ya dunia. 

Balozi Chen alibainisha kuwa China itaendelea kushirikiana na jumuiya ya kimataifa katika kusukuma mbele ajenda muhimu za maendeleo kama vile mabadiliko ya tabianchi, usuluhishi wa migogoro, na kukuza usawa duniani kupitia programu na majukwaa kama Belt and Road Initiative pamoja na Jukwaa la Ushirikiano wa China na Afrika (FOCAC). 

Katika salamu zake, Balozi huyo pia aliishukuru Serikali ya Tanzania kwa kuendeleza uhusiano wa muda mrefu uliopo kati ya nchi hizo mbili, akisisitiza kuwa uhusiano huo umejengwa katika misingi ya kuheshimiana, mshikamano na maendeleo ya pamoja. 

Hafla hiyo ya maadhimisho ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali, wawakilishi wa vyama vya siasa, mabalozi na wanadiplomasia kutoka mataifa mbalimbali, pamoja na wawakilishi wa mashirika ya kimataifa.






Chapisha Maoni

0 Maoni