Ridhiwani ashiriki kampeni kuwanadi wagombea wa CCM

 

Mgombea ubunge wa Jimbo la Chalinze kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ridhiwani Kikwete, ameendelea na mikutano yake ya kampeni kwa kishindo, ambapo ameshiriki kwenye uzinduzi wa kampeni za kunadi na kuomba kura kwa wagombea wa nafasi za Udiwani, Ubunge na Urais kwa tiketi ya CCM. Mkutano huo mkubwa umefanyika katika Kijiji cha Mihuga, Kata ya Miono, ndani ya Halmashauri ya Chalinze.

Akiongea mbele ya wakazi wa kijiji hicho, Ridhiwani Kikwete aliwataka wananchi kuendelea kuiamini CCM na kumuunga mkono kwa dhati mgombea urais wa chama hicho, Dkt. Samia Suluhu Hassan, akisisitiza kuwa rekodi ya utekelezaji wa Ilani ya CCM katika kipindi kilichopita ni ushahidi tosha wa uongozi bora.

“Tumeshuhudia maendeleo makubwa katika kipindi cha uongozi wa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuanzia miundombinu, elimu, afya, maji, hadi nishati. Haya yote yamewezekana kwa sababu ya uongozi imara wa CCM unaofanya kazi kwa kushirikiana,” alisema Ridhiwani huku akishangiliwa na wananchi waliohudhuria.

Aidha, Ridhiwani aliwakumbusha wananchi umuhimu wa kuchagua viongozi wote wanaotokana na CCM kuanzia ngazi ya Udiwani, Ubunge hadi Urais maarufu kama "mafiga matatu".

Ameeleza kuwa mafanikio makubwa ya utekelezaji wa Ilani yanatokana na mshikamano na ushirikiano kati ya viongozi hao, jambo linalowezesha serikali kutekeleza miradi ya maendeleo kwa ufanisi.

Mkutano huo ulihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa CCM wa ngazi ya wilaya na mkoa, pamoja na wapenzi na wanachama wa chama hicho waliokuja kuonesha mshikamano na kuunga mkono kampeni za chama chao kuelekea uchaguzi mkuu ujao.



Chapisha Maoni

0 Maoni