Mahakama Kuu yamrejesha Luhaga Mpina kuwania urais

 

Mahakama Kuu Masijala Kuu-Dodoma, imemrejesha kwenye mbio za kuwania nafasi ya urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mgombea urais wa chama cha ACT-Wazalendo Luhaga Mpina.

Katika hukumu yao, majaji wamesema Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) ni huru na haikupaswa kusikiliza maelekezo ya mtu au taasisi yoyote, ikiwemo Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa.

Katika kesi hiyo iliyokuwa inasikilizwa na jopo la majaji watatu, Abdi Kagomba, Evaristo Longopa na John Kahyoza, Mahakama Kuu pia wamesema kwa kutopokea fomu za Mpina, Tume ilimnyima haki ya kikatiba na ile ya kusikilizwa.

Vile vile Majakama Kuu imebatilisha barua ya Tume ya kumzuia Mpina kurejesha fomu kwa kuwa ilikuwa kinyume cha Katiba na haikuwa na nguvu ya kisheria.

Mahakama imeitaka Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) impe nafasi  mgombea huyo wa ACT-Wazalendo kuwasilisha fomu zake na mchakato uendelee ulipoishia Agosti 27, 2025.

Mpina alikuwa anapinga kuenguliwa katika mbio za urais kwenye Uchaguzi Mkuu wa 2025 ambapo INEC ilimzuia kuingia kwenye ofisi za tume kukabidhi fomu zake na kuteuliwa.

INEC ilichukua uamuzi huo, kutokana na taarifa ya Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, kuwa mgombea huyo hakukidhi vigezo vya kuteuliwa ndani ya ACT-Wazalendo, baada ya kupingwa na kada wa chama hicho.

Chapisha Maoni

0 Maoni