Waziri Ofisi ya Rais - Menejimenti ya
Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhiwani Kikwete amesema
Serikali itaendelea kuboresha maslahi ya watumishi wa umma nchini ili
kuongeza ufanisi wa taasisi za umma na kuleta huduma bora kwa
wananchi.
Akizungumza katika mkutano wa maafisa tawala na
maafisa rasilimali watu uliofanyika katika Ukumbi wa AICC mkoani
Arusha, Mhe. Ridhiwani amesema amewakumbusha watumishi hao kutekeleza
wajibu wao na kuleta furaha kwa watumishi wa umma ili nao waweze
kupeleka furaha na neema kwa Watanzania. Amesema hatua hiyo inatokana
na maamuzi mbalimbali yanayofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita kwa
lengo la kuboresha maslahi ya watumishi wa umma nchini.
Aidha,
Mhe. Ridhiwani amesema uamuzi wa hivi karibuni wa Serikali kupandisha
madaraja watumishi 219,042 ni hatua ya kihistoria katika kuimarisha
utumishi wa umma nchini. Hatua hiyo imepata ridhaa ya Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan.
Pia, amesema
Serikali imeongeza mishahara ya watumishi wa umma kwa asilimia 35.1
mwaka 2025 pamoja na kuongeza kima cha chini katika sekta binafsi kwa
asilimia 33.4 kwa mwaka 2025/26. Ameeleza kuwa maboresho hayo
yatazigusa sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu, kilimo, mawasiliano,
usafirishaji, nishati, viwanda, biashara, hoteli, michezo, uvuvi,
baharini, madini na utamaduni.
Kwa mujibu wa Waziri Mhe.
Ridhiwani Kikwete, matokeo ya kitakwimu yanaonyesha kasi ya mageuzi
ya kiutumishi chini ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais
Samia Suluhu Hassan, hali inayotafsiriwa kuwa ni uongozi wa kimkakati
unaoweka mbele ustawi wa watumishi pamoja na kuongeza ufanisi wa
taasisi za umma nchini.


.jpeg)
0 Maoni