Tanzania yazishukuru nchi za Afrika kwa jitihada za uhifadhi

 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, leo Julai 12, 2025, ameshiriki kikao maalum cha Kundi la Afrika (Africa Group) kilichofanyika pembezoni mwa Mkutano wa 47 wa Kamati ya Urithi wa Dunia ya Unesco unaoendelea jijini Paris, Ufaransa.

Kikao hicho ni sehemu ya mikakati ya pamoja ya nchi za Afrika katika kujadili na kujipanga kuhusu maeneo ya urithi wa dunia yanayopatikana barani humo, kwa lengo la kulinda maslahi ya Afrika wakati wa majadiliano ya pamoja na mabara mengine.

Mbali na Dkt. Abbasi, kikao hicho pia kimehudhuriwa na Balozi wa Tanzania nchini Ufaransa, Mhe. Ali J. Mwadini, pamoja na wataalamu mbalimbali kutoka Tanzania. Katika kikao hicho, Dkt. Abbasi na Balozi Mwadini waliwasilisha salamu za Serikali ya Tanzania na kutoa shukrani kwa Kamati hiyo pamoja na nchi wanachama wa Afrika kwa juhudi wanazozifanya kusaidia nchi za bara hilo katika kulinda maeneo yao ya urithi wa dunia.

Aidha, taarifa zinaeleza kuwa ripoti za hali ya uhifadhi wa maeneo ya urithi wa dunia kutoka Tanzania ambazo zilipaswa kuwasilishwa mwaka huu ikiwemo Ngorongoro, Selous na Kilwa, tayari zimepitishwa na kuidhinishwa na vikao vya Unesco.

Mkutano wa Kamati ya Urithi wa Dunia unaendelea jijini Paris na unatarajiwa kuhitimishwa mwishoni mwa wiki hii, ukiwa na ajenda mbalimbali kuhusu ulinzi na uhifadhi wa maeneo ya urithi wa dunia kutoka mataifa mbalimbali.





Chapisha Maoni

0 Maoni