Ripoti mpya ya Shirika la
Umoja wa Mataifa la Utalii (UN Tourism) kwa robo ya kwanza ya mwaka 2025
imeonesha Tanzania ikiendelea kung’ara katika sekta ya utalii, kwa kuongoza
Afrika kwa mapato na kuingia kwenye tatu bora ya nchi zenye ongezeko kubwa la
watalii barani.
Ripoti hiyo, iliyotolewa
mwishoni mwa Mei, imefanya tathmini ya mwenendo wa utalii duniani kwa
kulinganisha takwimu za mwaka huu na zile za mwaka 2019, kabla ya janga la
UVIKO-19 – ikiwa ni kipimo cha kuonesha urejeo wa hali ya kawaida na mafanikio
ya nchi mbalimbali katika sekta hiyo muhimu kiuchumi.
Tanzania Yatinga Tatu Bora Afrika kwa Ongezeko la
Watalii
Kwa mujibu wa ripoti
hiyo, Tanzania imepanda hadi nafasi ya tatu Afrika kwa ongezeko la idadi ya
watalii, ikiwa imeongezeka kwa asilimia 50 ikitanguliwa na Morocco (60%) na
Ethiopia (52%). Ongezeko hilo limeifanya Tanzania kuwa miongoni mwa nchi 20
bora duniani katika kipengele hicho, ikiungana na mataifa kama Brazil, Albania,
Qatar na Saudi Arabia.
Yashika Namba Moja Afrika kwa Ongezeko la Mapato
Katika upande wa mapato
yatokanayo na utalii, Tanzania imeibuka kidedea barani Afrika kwa kuongoza kwa
ongezeko la asilimia 66 ikilinganishwa na mwaka 2019. Imeizidi Tunisia (62%) na
Morocco (49%), na kushika nafasi ya 12 duniani, ikiweka jina lake sambamba na
mataifa tajiri kama Norway, Moldova, Brazil, Qatar na Saudi Arabia.
Dkt. Abbasi: Mbegu za Mikakati Zimezaa Matunda
Akizungumzia mafanikio
hayo akiwa Paris, Ufaransa, Katibu Mkuu wa Utalii na Mwenyekiti wa Kamati ya
Rais ya Kuitangaza Tanzania, Dkt. Hassan Abbasi alisema, “Haya ni matokeo ya
mikakati thabiti. Hatukuweza kuyapata haya kwa kukaa ofisini na kusubiri
miujiza.”
Dkt. Abbasi alieleza kuwa
mafanikio hayo ni zao la juhudi za viongozi mbalimbali akiwemo Rais Samia
Suluhu Hassan kupitia filamu za Royal Tour na Amazing Tanzania, pamoja na
ushiriki wa mabalozi, taasisi na wadau katika maonesho makubwa ya utalii
kimataifa.
“Mbegu hizo ndizo zimezaa
mavuno haya. Na sasa tunaangalia mbele zaidi – kutangaza nchi kwenye majukwaa
makubwa kama michezo na matamasha yanayovuta macho ya dunia, kama ilivyo kwa
Qatar na Saudia,” alifafanua Dkt. Abbasi.
Watalii Wafurika, Mapato Yavunja Rekodi
Akijibu kuhusu iwapo
takwimu hizo zinalingana na hali halisi nchini, Dkt. Abbasi alisema, “Nchi
imefurika watalii kila kona. Taarifa ya Benki Kuu (BoT) ya hivi karibuni
inaonesha utalii umeingiza dola bilioni 3.92 – ikishika nafasi ya kwanza kwa
kuchangia fedha za kigeni.”
Aliongeza kuwa taasisi
kubwa za utalii kama TANAPA, TFS, TAWA na Mamlaka ya Ngorongoro zimekusanya
mapato kwa kiwango ambacho hakijawahi kufikiwa tangu zianzishwe.
Akitolea mfano masoko
makuu ya nje, Dkt. Abbasi alitaja Marekani kuwa na ongezeko la watalii kwa
asilimia 41, huku China na India zikionesha ongezeko kubwa zaidi, China kwa
asilimia 108 na India asilimia 75.
“Kwa kifupi, kona zote
tunaona watalii wanaongezeka na mapato yanapanda. Narudia tena na shika sana
hili neno MIKAKATI,” alisisitiza.
0 Maoni