Ofa ya Sabasaba yaamsha hamasa ya utalii wa ndani Bagamoyo

 

Baadhi ya wananchi kutoka Mkoa wa Dar es Salaam na Pwani wamejitokeza kwa wingi kutembelea vivutio vya kihistoria katika mji mkongwe wa Bagamoyo, wakichochewa na elimu na ofa maalum ya utalii waliyoipata kupitia Banda la Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kwenye Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba.

Wakazi hao waliotembelea maeneo ya kihistoria wamesema elimu waliyoipata imewafungua macho kuhusu thamani ya utalii wa ndani na umuhimu wa kuhifadhi urithi wa taifa, huku wakieleza furaha yao baada ya kujionea vivutio hivyo kwa macho.

Agness Shayo, mmoja wa wageni waliotembelea Banda la TFS Sabasaba, alisema alihamasika kuja Bagamoyo baada ya kusikia simulizi za vivutio vya kipekee.

“Nilipoelezwa kuhusu Mbuyu wa Ajabu ambao ukiuzunguka unaongeza siku za kuishi, nilitamani sana kuona. Sasa nimeona kwa macho yangu na hata kushuhudia Kisima cha Miujiza ambacho hakikauki maji,” alisema Shayo kwa furaha.

Kwa upande wake, Brigiti Mahanga, mwanafunzi wa shule ya sekondari ya wasichana St. Alicia iliyoko Visiga, alisema ziara hiyo imeongeza uelewa wake kuhusu historia.

“Tunaambiwa sana kuhusu historia darasani, lakini kujionea kwa macho kunasaidia kuelewa zaidi. Ningependa wanafunzi wengi wapate fursa kama hii,” alisema na kuomba vivutio hivyo vilindwe kwa manufaa ya vizazi vijavyo.

Akizungumzia ongezeko la wageni msimu huu, Mhifadhi wa Eneo la Kaole, Bi Siyawezi Hungo, alisema kumekuwa na ongezeko la Watanzania wanaotembelea vivutio vya Bagamoyo hasa msimu wa Sabasaba, jambo linalodhihirisha mwamko mpya wa kuthamini utalii wa ndani.

“Watu wanapenda kujua historia yao na sasa tunashuhudia wengi wakifika kujifunza na kushangaa urithi huu wa zaidi ya miaka 800 iliyopita,” alisema Bi Siyawezi.

Magofu ya Kaole na Mji Mkongwe wa Bagamoyo umeendelea kuwa kitovu cha historia na urithi wa kiutamaduni nchini, kutokana na vivutio kama Kaburi la Wapendanao, Msikiti wa kale wa zaidi ya miaka 800, Mbuyu wa Ajabu na Kisima cha Miujiza, ambavyo vimekuwa kivutio kwa watalii wa ndani na wageni kutoka nje ya nchi, hasa wakati wa matukio makubwa ya kitaifa kama Sabasaba.



Chapisha Maoni

0 Maoni