Hakuna aliyeenguliwa kwenye mbio za udiwani, ubunge - Makalla

 

Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa Chama cha Mapinduzi (CCM), CPA Amos Makalla, amesema hadi sasa hakuna mwanachama yeyote aliyeenguliwa katika mchakato wa kuomba kugombea nafasi za Udiwani au Ubunge.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Julai 13, 2025 katika Ofisi za Makao Makuu ya CCM Jijini Dodoma, Makalla amesema taarifa zinazoenezwa kuwa baadhi ya wagombea wameenguliwa si za kweli na zinalenga kupotosha umma kuhusu mchakato wa ndani ya chama hicho.

“Naomba nisisitize, kwa utaratibu wetu wa Chama cha Mapinduzi, mpaka sasa hakuna mtu ambaye ameenguliwa au kukatwa kama ambavyo inaripotiwa kwenye vyombo vya habari. Nimeona wameandika huyu kapenya, huyu kafyekwa, huyu hayupo kwenye tatu bora... lakini mchakato huu bado unaendelea,” amesema Makalla.

Amefafanua kuwa kwa sasa Sekretarieti ya CCM inaendelea kupokea taarifa kutoka mikoa mbalimbali, na taarifa hizo zitawasilishwa kwenye vikao vya juu vya chama, likiwemo la Kamati Kuu ambako maamuzi ya mwisho yatafanyika.

Makalla amesema kwamba ni Kamati Kuu ya CCM pekee ndiyo yenye mamlaka ya kutoa orodha rasmi ya wagombea watakaokwenda kupigiwa kura za maoni.

“Kamati Kuu itakapohitimisha, tutatoka kuwaambia walioteuliwa kwenda katika kura za maoni ndani ya CCM. Zamani mlivyozoea ni kwamba kila mgombea alikuwa anapelekwa kwenye kura za maoni, lakini sasa tunachuja na kupitisha wachache tu kwa ajili ya kura hizo,” amesema.

Amesisitiza kuwa mchakato huo unazingatia taratibu za chama, na kuwahakikishia wanachama wote kuwa haki na usawa vitazingatiwa hadi mwisho wa mchakato huo.

Chapisha Maoni

0 Maoni