Nyota wa klabu ya
Barcelona na timu ya taifa ya Hispania, Pablo Gavi, amejiunga na orodha ya
wachezaji nyota wa kimataifa wanaochagua Tanzania kama sehemu ya mapumziko yao.
Kiungo huyo mahiri
yupo katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti pamoja na mpenzi wake, Ana Pelayo, akifurahia
mandhari na vivutio vya kipekee vya nchi.
Ujio wa Gavi unakuja
siku chache tu baada ya wachezaji wengine watatu wa soka kutoka Hispania kutua
nchini kwa mapumziko. Nyota hao ni pamoja na David Raya wa Arsenal, David De
Gea aliyewahi kung’ara Manchester United, na kiungo wa Barcelona, Pedri.
Hii inaongeza idadi
ya mastaa wa soka wanaotembelea Tanzania msimu huu wa kiangazi, hali
inayoendelea kuiweka nchi kwenye ramani ya kimataifa kupitia utalii.
Mbali na wachezaji
hao wa Hispania, Tanzania pia imepokea nyota wengine wawili maarufu duniani;
mshambuliaji wa zamani wa Sweden, Barcelona na AC Milan, Zlatan Ibrahimovic,
pamoja na Arnaut Danjuma, mshambuliaji wa Girona na timu ya taifa ya Uholanzi.
Tanzania imeendelea
kuvutia wageni maarufu kwa vivutio vyake vya kipekee kama Hifadhi ya Serengeti,
Mlima Kilimanjaro na Visiwa vya Zanzibar, huku mastaa hao wakichangia kuiweka
nchi kwenye jicho la dunia kupitia mitandao ya kijamii na vyombo vya habari vya
kimataifa.




0 Maoni