Mradi JNHPP wakamilika, kutoa uhakika wa umeme nchini - Majaliwa

 

Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa ameliambia bunge kuwa mradi wa uzalishaji umeme katika Bwawa la Julius Nyerere (JNHPP) umekamilika na tayari megawati 2,115 zimeunganishwa kwenye gridi ya taifa na kuongeza kiwango cha umeme kufikia megawati 4,031.7.

Mhe. Majaliwa amesema kwamba kuanza kwa uzalishaji wa umeme katika mradi huo kumeongeza kiwango cha upatikanaji wa umeme wa uhakika na kuwa chachu ya kasi ya maendeleo ya nchi. 

“Hadi Machi 2025, jumla ya megawati 2,115 zimeunganishwa kwenye gridi ya taifa na hivyo kuongeza kiwango cha umeme katika gridi ya taifa kufikia megawati 4,031.7, alisema Mhe. Majaliwa.

Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa ameeleza hayo wakati akisoma Hotuba ya Bajeti ya Ofisi yake na Bunge 2025/26 leo Aprili 9, 20225, na kusema Serikali inaendelea kukamilisha ujenzi wa mradi wa uzalishaji umeme katika Bwawa la Julius Nyerere kwa gharama ya shilingi trilioni 6.6.

Amesema kuwa katika kipindi cha Novemba, 2020 hadi Februari, 2025, Serikali pia imeunganisha umeme katika vijiji 4,071 kwa gharama ya shilingi bilioni 1,593 na hivyo kuwezesha vijiji vyote 12,318 vya Tanzania Bara kuunganishwa na umeme.

Ameeleza kuwa hatua inayofuata baada ya kukamilisha mradi wa kupeleka umeme katika vijiji vyote, ni kupeleka umeme kwenye vitongoji ambapo jumla ya vitongoji 33,657 kati ya 64,359, sawa na asilimia 52.3 vimeunganishwa na huduma ya umeme.

Mhe. Majaliwa amesema kwamba usambazaji wa umeme katika vijiji na vitongoji utawezesha wananchi kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi hususan zinazohitaji nishati ya umeme zikiwemo kuchomelea vyuma, useremala, kuchakata nafaka na kuchenjua madini.




Chapisha Maoni

0 Maoni