Naibu Katibu Mkuu Maliasili na Utalii atembelea Msitu wa Hifadhi Bondo

 

Serikali inaendelea na juhudi za kulinda rasilimali za misitu nchini, ambapo Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii anayeshughulikia Maliasili, CP Benedict Wakulyamba, leo ametembelea Msitu wa Hifadhi wa Bondo uliopo kati ya Wilaya ya Handeni na Kilindi.

Ziara hiyo iliyofanyika jana imelenga kutathmini utekelezaji wa hatua za kulinda hifadhi hiyo dhidi ya uvamizi na uharibifu wa mazingira.

Katika ziara hiyo, CP Wakulyamba aliambatana na Kamishna Msaidizi wa Kanda ya Kaskazini, SACC James Nshare, pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Kilindi, DC Hashim Mgandilwa, wahifadhi wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kutoka Handeni na Kilindi, na viongozi wa usalama wa eneo hilo.

Ziara hiyo imejikita katika kukagua maeneo yaliyowahi kuwa na makazi ya watu waliovamia hifadhi hiyo na tathmini ya utekelezaji wa zoezi la kuwaondoa (eviction). Aidha, ameangalia mipaka ya msitu wa Bondo, uwekaji wa mabango ya hifadhi, na mikakati ya kudhibiti uharibifu wa mazingira.

“Serikali haitarudi nyuma katika kulinda misitu yetu dhidi ya uharibifu. Hifadhi ya Bondo ni mojawapo ya maeneo muhimu ya bioanuwai, na tunahakikisha kuwa sheria za uhifadhi zinatekelezwa ipasavyo,” alisema CP Wakulyamba wakati wa ukaguzi huo.

Msitu wa Bondo, ambao ni mojawapo ya vyanzo muhimu vya maji na makazi ya viumbe hai, umeendelea kukabiliwa na changamoto za uvamizi na ufyekaji miti. Ili kuhakikisha hifadhi hiyo inalindwa, Serikali imeweka kambi maalum ya ulinzi katika eneo la Gongoki, ambapo askari wa TFS wameimarisha doria za mara kwa mara.

Katika ziara hiyo, CP Wakulyamba ametembelea vituo vikuu vitatu vya kijiji cha Bondo vilivyokuwa na makazi kabla ya utekelezaji wa hatua za uhifadhi, ambavyo ni Chelekachakomba, Doro Centre, na Gongoki.

Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii inaendelea kutekeleza mikakati madhubuti ya uhifadhi, ikiwa ni pamoja na:

                             Kuimarisha doria na udhibiti wa uvamizi wa misitu kwa kutumia askari wa TFS na vyombo vya usalama.

                             Uwekaji wa alama na mabango ya mipaka ili kuzuia uingizwaji holela wa watu katika hifadhi.

                             Kuhamasisha jamii zinazozunguka hifadhi kushiriki katika kulinda rasilimali za misitu kupitia programu za elimu ya uhifadhi.

Juhudi hizi ni sehemu ya utekelezaji wa sera za uhifadhi wa mazingira na misitu ili kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi na upotevu wa bioanuwai.




Chapisha Maoni

0 Maoni