Vyombo vya habari vyahimizwa kutumia Kiswahili sahihi

 

Naibu Waziri wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Hamis Mwinjuma amevitaka vyombo vya habari nchini kuwa mstari wa mbele katika kutumia Kiswahili sahihi, ili kujenga jamii inayozungumza lugha fasaha ya Kiswahili.

Mhe. Mwinjuma ametoa kauli hiyo jana Februari 14, 2025 Jijini Dodoma wakati akifunga Mkutano wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji 2025 uliofanyika kwa siku mbili kuanzia Februari 13-14, 2025.

“Ni rai yangu kwenu kwa kuwa nyinyi ndio wenye jukumu la kwanza kabisa la kuhakikisha matumizi sahihi ya Kiswahili ndio yanayoshika hatamu.. Kiswahili sahihi kinatumika katika vyombo vya habari na hivyo kuambukiza jamii yeu,” alisema Mhe. Mwinjuma.

Pamoja na mambo mengine, Mhe. Mwinjuma alipongeza mkutano huo kuzungumzia mada mbalimbali muhimu zikiwemo za Sheria na kanuni za uchanguzi mkuu pamoja na matumizi sahihi ya akili unde na kusema kwamba milango ya wizara ipo wazi wakati wowote kwa vyombo vya habari.

Amewataka waandishi wa habari kutumia mafunzo waliyopatiwa katika mkutano huo kuripoti uchangizi mkuu wa 2025 kwa weledi wa hali ya juu na kutenda haki ili wananchi wapate taarifa na kuwawezesha kufanya maamuzi sahihi.

Amesema kupitia vyombo hivyo wananchi wanapata taarifa sahihi za wagombea zinazowawezesha kufanya maamuzi kwa mustakabali wa nchi hivyo vina umuhimu katika uchaguzi ujao wa Oktoba mwaka huu.

Kwa upande wake Meneja wa Kitengo cha Huduma za Utangazaji (TCRA), Mhandisi Andrew Kisaka aliwapitisha washirika katika kufahama kanuni za utangaji za uchaguzi, na kusisitiza vyombo vya habari kutenda haki kwa vyama vyote.

“Vyombo vya habari vinapaswa kutenda haki kwa kutoa habari kwa usawa kwa wagombea wote wa  vyama vyama vya siasa bila upendeleo wowote wakati wa uchaguzi mkuu,” alisisitiza Mhandisi Kisaka.

Amesema hata katika taarifa za habari kila chama kinapaswa kuwa na habari ya kwanza na sio kila siku chama kimoja tu ndio kinakuwa na habari ya kwanza (lead story) na kuwataka waandishi wa habari wajikite zaidi katika sera za vyama na ahadi za wagomea.

“Muepuke kuripoti habari za wagombea za matusi na lugha za uchochezi, bali mjikite katika kutoa habari za sera na ahadi za wagombea, pia mjiepushe kuongeza maneno yenu kwenye habari za kampeni wakati wa uchaguzi,” alisema Mhandisi Kisaka.

Ameeleza kwa vipindi vya mahojiano wagombea wote wa urais wanapaswa kufanyiwa kwa usawa na iwapo kuna mdahalo wa wagombea urais, wagombea washindane kwa Ilani za vyama vyao, Sera na ahadi na wala sio malumbano, na muongozaji hapaswi kuongeza neno lolote baada ya kumalizika mdahalo.

Mkutano huo ulioandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) unaofanyika Jijini Dodoma unakauli mbiu isemayo, “Wajibu wa Vyombo vya Utangazaji Kuelekea Uchaguzi Mkuu”.

Chapisha Maoni

0 Maoni