Kampuni binafsi za ulinzi Mwanza zatakiwa kuzingatia Sheria na Kanuni

 

Jeshi la Polisi mkoa wa Mwanza limewataka wamiliki wa kampuni binafsi za ulinzi mkoani humo kufuata sheria kwa kuwasimamia vyema askari wanaowaajiri kufanya kazi ya ulinzi katika maeneo mbalimbali.

Kauli hiyo imetolewa na Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Ramadhani Sarige kwenye kikao kazi na wamiliki hao ndipo akawahimiza kuhakikisha wanaweka utaratibu mzuri wa kutoa mafunzo kwa walinzi ili kuleta uelewa wa pamoja na kuimarisha nidhamu kwa askari hao wakati wanapotekeleza majukumu ya ulinzi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Upelelezi Makosa ya Jinai Mkoa wa Mwanza, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi (SSP), Yesaya Suddy akitoa elimu katika kikao hicho amesema katika jamii si ajabu kukutana na mlinzi anayelinda mali yenye thamani ya zaidi milioni mia tano lakini hajui hata kutumia silaha aliyonayo kwenye lindo kitu ambacho ni hatari kwa usalama.

Naye, Mwenyekiti wa Chama cha Ulinzi Rasilimali Watu Kanda ya Ziwa (TAMASCA), Charles Chacha amesema; "Elimu tuliyopata leo ni nzuri na itatusaidia sisi wakurugenzi wa makampuni ya ulinzi binafsi kutenda kazi zetu za kila siku kwa kuelimisha wajibu wa walimzi wetu namna ya utendaji wa kazi zao wanapokuwa lindoni."

"Tumekumbushwa kuhakikisha tunafata taratibu zote za ajira hususan katika kuwalipa walinzi mishahara kwa wakati kwa kufuata viwango vilivyowekwa na Serikali, kuwapa mikataba ya kazi za ulinzi na kupeleka michango yao NSSF," ameongeza Bw. Chacha.



Chapisha Maoni

0 Maoni